Akizungumza katika mikutano ya hamasa ya uchaguzi inayoendelea mkoani Singida, Bi. Nakomolwa amesema jukumu la wazazi ni kuhakikisha hakuna mwananchi anayeachwa nyuma katika kushiriki maamuzi ya mustakabali wa Taifa.
“Tuwasaidie kwa upendo na uaminifu. Tusiwaache nyuma wazee, walemavu, na wale wasiojua kusoma. Kila mmoja anastahili kushiriki katika mchakato wa demokrasia kwa mujibu wa sheria,” amesema Bi. Nakomolwa.
Amesisitiza kuwa msaada wowote unaotolewa katika vituo vya kupiga kura lazima uzingatie maelekezo ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ili kulinda uhalali wa kura na kuepusha uvunjaji wa taratibu.
Kwa mujibu wa Nakomolwa, wazazi wa CCM wanapaswa kuwa mfano bora wa uaminifu, heshima na umoja, na kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa amani, huku wakisisitiza sera za maendeleo zilizoletwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Kura ya kila Mtanzania ni sauti ya maendeleo. Ni wajibu wetu kuhakikisha kila mtu anaitumia vyema. Ushiriki wa wote ndio ushindi wa CCM na mustakabali wa Taifa letu,” amesisitiza.
Bi. Nakomolwa alihitimisha kwa kuwataka wananchi wa Singida kuendelea kuwa watulivu, wamoja na kuipigia kura CCM ili kuendeleza kasi ya maendeleo iliyoonekana katika sekta za elimu, afya, maji, na barabara katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.
“CCM ni chama cha watu wote, chama cha maendeleo. Tukipige kura kwa amani, tushirikiane kama familia moja – kwa pamoja tunalinda amani, tunajenga ushindi wa CCM 2025,” alimalizia kwa msisitizo.
0 Comments