![]() |
Uchunguzi wa maoni uliofadhiliwa na Shirika la Nation Media Group wikiendi iliyopita unaonyesha kuwa wagombea urais hao wawili wana umashuhuri sawa wa asilimia 42 kila mmoja.
Uchunguzi huo wa maoni unaonyesha kuwa uchaguzi wa rais wa Agosti nane utakuwa kimsingi ni mchuano baina ya Ruto wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) na Raila wa Muungano wa Azimio la Umoja One Kenya.
Wagombea wengine wote wa urais kwa pamoja wana umashuhuri wa asilimia moja tu katika uchunguzi huo wa maoni uliofanywa Mei 8-9 na Shirika la Infotrak Research and Consulting.
Hali kadhalika uchunguzi huo wa maoni umebaini kuwa asilimia 10 ya wapiga kura bado hawajaamua kuhusu mgombea wanayemtaka huku wengine asilimia 5 wakikataa kujibu swali hilo. Kwa msingi huo, asilimia 15 ya wapiga kura waliosalia watakuwa muhimu katika kuamua rais ajaye wa Kenya punde watakapochukua maamuzi.
![]() |
Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya |
Uchunguzi wa maoni uliofanywa na mashirika mengi katika kipindi cha miezi sita iliyopita unaonyesha kuna uwezekano mkubwa uchaguzi ukaingia duru ya pili kwani itakuwa vigumu kwa Ruto au Raila kupata zaidi ya asilimia 50 ya kura zinazohitajika ili kutangazwa mshindi katika duru ya kwanza.
Aidha uchunguzi huo umebaini kuwa pamoja na kuwa Rais Uhuru Kenyatta ambaye ni kutoka eneo la kati mwa nchi ametangaza kumuunga mkono Raila Odinga lakini asilimia 60 ya wakazi wa eneo hilo wanamuunga mkono Ruto.
0 Comments