WAZIRI BASHE ATOA MAAGIZO KWA RC, KILIMO CHA MKONGE

 

Waziri Bashe akizindua kitabu cha mwongozo wa mfuko wa wakfu (SDTF) kwa maendeleo ya walipa kodi kwa wadau wa mkonge.
Mkurugenzi mkuu wa Bodi ya Mkonge Tanzania(TSB) akitoa taarifa.

**********************

Na Hamida Kamchalla, KOROGWE.

MKUTANO wa Nne wa Wadau wa Sekta ya Mkonge Tanzania (TSB) umezinduliwa sambamba na Mfuko wa Wakfu (SDTF) kwa Maendeleo ya Walipa kodi wa Sekta ya Mkonge ambao umefanyika wilayani Korogwe, Mkoa wa Tanga.

Katika mkutano Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amemuaiza mkuu wa Mkoa wa Tanga Waziri Kindamba kusimamia suala la ugawaji wa viwanja kwa ajili ya makazi ambavyo ni maalumu kwa ajili ya kilimo katika halmashauri zote mkoani humo.

"Hatari kubwa ninayoiona, ni viongozi tuliopewa dhamana ya kumsaidia Rais, katika ngazi ya halmashauri tunakumbuka eneo la kilimo wakati wa kukusanya ushuru, tuna tatizo kubwa la kujadili bila kujadili umasikini, mkuu wa Mkoa mkalisimamie suala hili" amesema.

"Kwahiyo kuna umuhimu wa sisi kama serikali kukaa na kujadili kwa kina juu ya umasikini ili mapato ya serikali yapatikane kuliko kukimbilia kujadili mapato" alibainisha Bashe.

Katika baadhi ya Wilaya ambazo zimepata tatizo la wananchi kukosa mashamba ambayo yalitwaliwa na halmashauri ni Muheza na Mkinga ambapo, Bashe alimtaka mkuu wa Mkoa kufuatilia kwa ukaribu na kurudisha maeneo hayo kwa wakulima.

"Mfano leo asilimia kubwa ya mapato kwa Wilaya ya Mkinga inatokana na samaki, siku wavuvi wakaamua kuweka pembeni boti zao hawaendi kuvua hakuna mapato,

"Na kwa Wilaya ya Muheza, mimi nikuombe mkuu wa Mkoa wakati Waziri mkuu Kassim Majaliwa anatoa maelekezo ulikuwepo, mashamba yale yalirudishwa halmashauri lakini ni kwa ajili ya kilimo cha mkonge na siyo kuwana vina viwanja" amesema.

Waziri Bashe amesisitiza kwamba, "kwahiyo mimi nitaomba Mh. Rc hili ukalisimamie, hatuwezi kugawa viwanja vya kujenga kwenye eneo la kilimo haiwezekani, kama halmashauri inaona kulima mkonge hapafai basi walime zao jingine kwenye lile eneo".

Mkuruenzi mkuu wa Bodi ya Mkonge Tanzania (TSB), Saddy Kambona amesema wakati anakabidhiwa ofisi za Mkonge mwaka 2019 uzalishaji ulikuwa wastani wa tani 36,000 lakini kwa juhudi za serikali waliweza kuzalisha tani 48,000 mwaka 2022.

"Matarajio yetu kwa mwaka 2023 ni kuongeza uzalishaji kufikia tani 60,000 na tulivyotathmini uzalisaji wetu mpaka kufikia nusu ya mwaka huu tayari tumeshazalisha tani 34,000, hivyo tunapoenda kufunga mwaka tunaona kabisa tunakimbilia lengo la serikali la kuzalisha tani 120,000 ifikapo mwaka 2025 /26" amesema.


"Hii ni sehemu tu ya kuchangia ukuaji wa sekta ya kilimo ambapo ikifika mwaka 2030 kilimo kikue na kufikia wastani wa asilimia 10, na tunaona jitihada kubwa ambazo Wizara ya Kilimo zinazofanya kufikia kwenye mlengo huu".


Aidha Kambona amebainisha kwamba kupitia juhudi hizo, soko la zao hilo limeimarika na wakulima wengi waliojiuga kwenye Vyama vya Ushirika (Amcos) katika Wilaya ya Korogwe wamekuwa wakinufaika na bei hizo.


"Na Amcos hizi tumekuwa tukizitumia kama mfano kwa Amcos ambazo tunaendelea kuzisajili kadi wakati unavyokwenda, zinafanya vizuri na katika kipindi hiki cha miaka mitatu zimeweza kupewa mikopo ya matrekta kutoka benki ya NMB na kurejesha,


"Lakini pia benki ya NMB imewaamini sana wakulima wetu na sasa wamezishika Amos zote 5 na wanataka kuwapa tena mikopo ya bilioni 20 kwa ajili ya mashine za kuchakata mkonge (korona)" amebainisha.


Kambona amebainisha kwamba Amcos zilizopo wilayani Korogwe ni Magunga, Mwelya, Hale, Mgombezi na Magoma.

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments