MWENEZI WA CCM MKOA WA SINGIDA AWATAHADHARISHA WANACHAMA KUHUSU UCHUKUAJI WA FOMU

Zoezi la kuchukua fomu za kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) limeanza rasmi huku Mwenezi wa CCM Mkoa wa Singida, Ndugu Eliphasi Lwanji, akitoa wito mzito kwa wanachama wote kuzingatia taratibu na maadili ya chama katika hatua hiyo ya mwanzo ya mchakato wa uchaguzi.

Lwanji amebainisha kuwa zoezi hilo litadumu kwa siku tano tu, na amesisitiza kuwa hakuna haja ya bwembwe au kampeni za aina yoyote wakati wa kuchukua fomu, kwani hatua hiyo si kampeni bali ni sehemu ya mchakato wa kawaida wa kidemokrasia ndani ya chama.

"Zoezi la kuchukua fomu ni la kawaida, siyo kampeni. Wanachama wote wenye sifa wanayo haki ya kuchukua na kuchaguliwa bila bughudha yoyote," amesema Lwanji.

Kwa upande mwingine, vijana wa CCM mkoani Singida wametajwa kuwa wameandaliwa vizuri na kufundwa vya kutosha kwa ajili ya kushiriki kikamilifu katika usimamizi na uhamasishaji wa uchaguzi huo, wakilenga kudumisha nidhamu, amani na mshikamano ndani ya chama.

Mwenezi huyo pia amesisitiza kuwa mchakato mzima wa uchaguzi utafanyika kwa haki, na uteuzi wa wagombea utafanyika kwa kuzingatia taratibu rasmi za chama, kwa lengo la kupata viongozi bora, wenye uwezo wa kusimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM na kutetea maslahi ya wananchi.




 Na Mwandishi wetu Singida

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments