WANANCHI WA SIHA WASHUKURU SERIKALI KUTEKETEZA NZIGE

 Wananchi wa wilaya ya Siha mkoa wa Kilimanjaro wameipongeza serikali kwa hatua iliyochukua kudhibiti makundi ya nzige waliovamia maeneo ya mashamba ya kufuatia zoezi la kuangamiza nzige hao waliovamia mashamba yao hivi karibuni.

Wakizungumza na waandishi wa habari leo baadhi ya wakulima  walimweleza Naibu Waziri wa Kilimo Hussein Bashe aliyetembela mashamba ya Nanai eneo la Sanya Juu wilaya ya Siha kufuatilia kazi ya kuangamiza nzige ikiwa ni  leno la serikali kulinda maisha ya watu na mali zao.

Mzee Felix Mosha mkulima na mmiliki wa shamba la Kafori West Kilimanjaro alisema tukio la kuvamiwa na nzige juzi lilileta taharuki kwa wakazi wa maeneo hayo kwa kuwa sasa ndio wameanza kupanda mazao mashambani lakini wamefarijika kuona hatua za serikali chini ya wizara ya Kilimo kuwadhibiti  nzige  hao.

“Tunaishukuru serikali kwa kuja kwa haraka, leo tumeona wataalam wamefanikiwa kuwaangamiza nzige waliovamia mashamba yetu ya makademia na ngano  yanaendelea kuwa salama” alisema Mzee Mosha.

Naye mkulima Hassan Gonga anayemiliki shamba la Nanai wilaya ya Siha alisema mara baada ya wadudu hao kuvamia shamba lake la makademia waliwatafiti wadudu hao na kugundua kuwa hawapendi kelele hivyo wakaweka vifaa vya kupiga kelele shambani hapo hali iliyosababisha nzige hao waondoke kwenda msituni na kuliacha shamba likiwa salama bila madhara.

Akizungumzia operesheni kuangamiza nzige, Naibu Waziri Kilimo Hussein Bashe alisema mpaka sasa hali ya kuangamiza nzige tangu walipovamia maeneo ya Tanzania inaendelea vizuri na wadudu wamedhibitiwa kwa kupuliziwa viuatilifu kuwaua  kwa njia ya ndege na mabomba ya kushikwa kwa mikono.

Bashe alisema  kuwa wizara inatambua wilaya ya Siha ni muhimu kwa kilimo hivyo lazima itazamwe kwa karibu nzige wasije haribu ndio maana wanaendelea kwenda kujionea kazi ya kuwadhibiti nzige hao ambapo ameshuhudia makundi ya nzige waliokufa baada ya kupuliziwa sumu.

Bashe aliongeza kusema wizara imeongeza vifaa vya kusaidia kupambana na nzige pia imeanzisha mafunzo kwa maafisa ugani wa vijiji na kata kutambua aina za nzige ili iwe rahisi kudhibiti pale watakapojitokeza kwenye maeneo yao

“Mpaka sasa Longido tumefanikiwa kwa asilimia 95 zoezi limefanikiwa hakina masalia ya nzige ambapo nzige waliovamia Siha walitokea Longido baada ya kundi lao kupuliziwa sumu  hivyo wakakimbia na sasa tumewafuata hapa Sanya Juu tumewaua? Alisema Bashe.

Bashe aliongeza kusema kazi ya kudhibiti nzige wilaya ya Simanjiro imeenda vizuri ambapo hadi sasa taarifa za wataalam zinaonesha kumebakia kundi moja lililolojificha kwenye milima na kazi ya kulifuatilia ili liangamizwe.

“Hadi sasa hakuna madhara yoyote kwenye mazo ya wakulima tanagu nzige wavamie nchi hapa mwezi Janauri mwanzoni. Ni heri tupate madhara ya kufa kuku lakini nzige lazima tuwatafute kokote waliko “ alisisitiza Waziri Mkenda

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Teknolojia za visumbufu Taasisi ya Udhibiti wa Viautilifu kwenye Ukanda ywa Kitropiki (TPRI) Mhandisi Julius Mkenda alieleza kuwa kundi la nzige lililovamia wilaya ya Siha ni baadhi ya waliokimbia Longido baada ya kazi ya kunyunyizia kiuatilifu tarehe 22 mwezi huu hivyo wakatoroka na kuingia Siha na kuwa siyo kundi jipya kwa mujibu wa utafiti waliofanya.

Mhandisi Mkenda alibainisha kuwa nzige waliovamia Siha wanaendelea kuangamizwa kwa kutumia ndege maalum pia mabomba ya kupuliza kwa miko kwa wale walio jirani na makazi ya watu ambapo zoezi limeenda vema jana na leo na kuwa wataendelea kuchukua hatua za kuwadhibiti .

“Jambo kubwa kwa Siha ni kuwa nzige hawa wana siku tatu tayari wameanza kuwa wa njano toka wekundu hali amabyo  ni hatari hivyo sasa tunawafundisha maafisa ugani wa kata na vijiji wajue namna ya kuwatambua na kuwadhibitipindi wakijitokeza tena” alisisitiz Mhandisi Mkenda.

Waziri wa Kilimo pamoja na Naibu Waziri wa Kilimo wapo kwenye mikoa ya Arusha na Kilimanjaro kufanya ufuatiliaji wa karibu wa udhibiti wa makundi ya nzige ili wasije haribu mashamba ya wakulima.

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments