Karagwe. Diwani wa kata ya Kibondo wilaya ya Karagwe, Maginus Cheusi amehoji sababu ya wanawake wajawazito kulipia kias cha sh 300,000 wakati wa kujifungua kwa oparesheni.
Ametoa kauli hiyo leo Machi 9 katika kikao cha kawaida cha baraza la madiwani la kupitisha bajeti ya mwaka 2021/2022.
Amesema kuna mkanganyiko wa maelezo kuhusu wanawake wajawazito na watoto walio chini ya miaka mitano, hivyo itolewe kauli itakayoondoa sintofahamu hiyo.
"Mwenyekiti naomba kwa ruhusa yako nipate maelezo kama wajawazito wanatakiwa kulipa fedha wakati wa kujifungua, maana kwenye vyombo vya habari tunasikia wanaeleza hawalipii, lakini kwangu kwenye hospital ya Nyakaiga wajawazito wanalipia Sh300,000 ," amesema Cheusi.
Kufuatia ombi hilo mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Karagwe Wallesi Mashanda alimwelekeza Mganga mkuu wa Wilaya ya Karagwe Dk Ramadhani Hussein kuandaa taarifa za fedha za mfuko wa pamoja zilizotolewa na zimetumikaje.
Kwa upande wake Mganga mkuu wa halmashauri ya Karagwe Dk Ramadhani Hussein amehaidi kuandaa mchanganuo huo na taarifa itolewe kwa wakati.
0 Comments