SUALA LA WAAMUZI LITAFUTIWE SULUHISHO

Kumekuwa na kasumba ya mashabiki, makocha pamoja na wachezaji kuwageukia waamuzi na kuwabebesha zigo la lawama pale wanapokwama kupata matokeo ama wakati mwingine wanaposhinda.


Kwa kuwa kelele kwa waamuzi kwa sasa zimekuwa zikizidi kila leo ni muhimu kwa mamlaka kuweza kulichukulia hili suala kwa uzito wa kipekee kwani linatibua utamu wa ligi.


Wengi wanaokwenda uwanjani hawapendi kuona makosa ya kizembe yakitokea na kwa waamuzi inabidi watambue kwamba pale ambapo wanaamua hakuna anayeweza kufanya mabadiliko hapo baadaye.


Kutokana na kasi ya mechi kuwa kubwa kwa sasa nadhani kuna umuhimu wa Shirikisho la Soka Tanzania,(TFF) kuangalia namna ya kufanya kuweza kuliondoa kabisa hili tatizo la kelele za waamuzi.


Ipo wazi waamuzi wanafanya kazi yao vizuri kwa kufuata sheria 17 ila kuna wakati wanapata kigugumizi kwa kutaka kuweka usawa kwa sababu ya makosa ambayo yamepita ama kushindwa kuelewana ndani ya uwanja hili sio sawa.


Kwa wale ambao watapewa jukumu la kusimamia mechi zote itapendeza wakifuata sheria 17. Ikiwa mchezaji anastahili kupewa kadi nyekundu kwa mujibu wa sheria na apewe hata kama itakuwa ni kwa timu nzima haki itendeke.


Pia sehemu ya penalti hata kama ikitokea timu ikapata penalti tatu hata saba zifunikwe na zipigwe tu hakuna haja ya kuhofia eti manenomaneno ama presha ya mchezo hiyo hakuna.

Wapo waamuzi ambao wanafanya kazi zao vizuri sasa hawa kazi yao nzuri inapotezwa na baadhi ambao wanavurunda kwa kukusudia ama bahati mbaya.

Wachezaji wakiwa ndani ya uwanja wana kazi kubwa ya kutafuta matokeo ila inapotokea wanakwamishwa na juhudi za mwamuzi haileti picha nzuri.


Wakati uliopo na kwa mechi zinazofuata itakuwa vizuri waamuzi wakafanya kazi yao bila presha ama shinikizo katika maamuzi yao ndani ya uwanja.

Ipo wazi na inaonekana kwamba msimu huu kwa kuwa timu ni chache ushindani utakuwa mkubwa. Hivyo waamuzi nao pia wajipange kwenda sawa na kasi ambayo ipo ndani ya uwanja.


Mzunguko wa pili umeanza kwa utofauti ndani ya ligi ambapo kila timu imekuwa ikipambana kusaka ushindi kwenye mechi ambazo itacheza.


Kutokana na ushindani huo ni muhimu kwa timu pamoja na wachezaji kuendelea kujipanga vizuri. Hakuna timu ambayo inaweza kukubali kupoteza mchezo ilihali inahitaji ushindi.

Inahitajika umakini mkubwa kwa waamuzi katika kutoa maamuzi yao. Ni wazi kwamba kwa sasa kila mchezaji amekuwa akitafuta sababu pale timu inapokwama kushinda.


Wengine wamekuwa wakiangukia kuwapa lawama waamuzi huku wengine wakidai ni kutokana na miundombinu kutokuwa rafiki.


Jambo la msingi kwa sasa ni kila mmoja kutimiza majukumu yake kwa usahihi uwanjani hilo litafanya zile kelele na lawama kupungua.


Waamuzi kwa nafasi ambao wanapewa kufanya kazi ni muhimu kufanya kazi kwa juhudi na kutimiza zile sheria 17 za mpira na itafanya ligi izidi kuwa imara.

Uimara wa ligi utafanya maendeleo ya soka letu kuzidi kupanda kila wakati na hilo ni faida kwa taifa letu kiujumla kwa kuwa mafanikio yanatuhusu sisi wenyewe.

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments