Tanga. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Ummy Mwalimu amesema atazifumua sekretariet za mikoa zisizotekeleza majukumu yake ipasavyo.
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari leo, Jumanne Aprili 27, 2021 na Tamisemi imeeleza Waziri Ummy ambaye pia ni mbunge wa Tanga Mjini ameeleza hayo wakati akizungumza na sekretariet ya mkoa jijini humo.
Katika maelezo yake, Waziri Ummy amesema jicho lake la karibu litakuwa ni sekretarieti za mikoa akisema hataki kuanza kupambana na halmashauri 184 wakati kuna watu kwenye sekretarieti za ambao hawataki kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
Hawa wako karibu kimazingira na kiutendaji na halmashauri hizo ninataka watekeleze majukumu yao ipasavyo na mimi nipate taarifa zote kutoka kwao. Sitaki kuona sekretarieti za mikoa ni watu wa ku-compile’ taarifa za halmashauri tu ninataka kuona inakaa na halmashauri zao zinawashauri, na kuweka mambo pamoja kuzisimamia ipasavyo,” amesema waziri Ummy.
Mbali na hilo, waziri huyo amezitaka sekratariet za mikoa kusimamia ukusanyaji wa mapato ya halmashauri zilizoko kwenye maeneo yao matumizi ya fedha za mapato ya ndani ikiwa ni pamoja na kupeleka fedha hizo kwenye miradi ya maendeleo na utoaji wa mikopo ya asilimia 10.
Katika hatua nyingine, Waziri Ummy alikabidhi hundi ya Sh300milioni kwa vikundi 37 wa jiji la Tanga ikiwa ni mkopo wa asilimia 10 iliyotolewa na jiji hilo kupitia mapato ya ndani ya robo tatu ya mwaka 2020/21.
0 Comments