Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linawashikilia watu 13 kwa tuhuma ya kujipatia pesa kwa njia ya udanganyifu wa kuuza madini ya bandia.
Jeshi hilo linawashikilia watuhumiwa wengine wanne kwa kuiba pikipiki.
Taarifa iliyotolewa leo Jumanne Agosti 24, 2021 na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, Jumanne Muliro imesema kuwa Agosti 20, saa tisa alasiri maeneo ya Mbezi Makonde Wilaya ya Kinondoni walikamatwa watuhumiwa 13 wakiongozwa na Christopher Robert@Mayanga, (29), Mkazi wa Tabata Bima na Harold Martin@Pouwes,(60) raia Afrika Kusini na wenzao 11 kwa tuhuma za kujipatia pesa kwa njia ya udanganyifu wa kujihusisha na uuzaji wa madini bandia.
Amesema uchunguzi wa shauri hilo unakamilishwa kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola na watafikishwa mahakamani haraka iwezekanavyo.
“Watuhumiwa hao walikutwa na boksi nne zenye madini bandia zinazodhaniwa kuwa ni dhahabu, mitambo miwili inayodaiwa ni ya kuyeyushia madini, kifurushi kimoja
cha madini bandia, vipande saba vya madini bandia, Pasport tano za kusafiria nchi mbalimbali wakijifanya ni wafanya biashara wa kimataifa,”amesema.
Amebainisha kuwa watuhumiwa hao wamekutwa na magari sita waliyokuwa wanayatumia kufanyia vitendo hivyo vya utapeli.
Ameyataja magari hayo ambayo yanachunguzwa kuwa ni T 479 DHW Toyota Prado, T 740 DSW Toyota Alphard, T 273 DHM Toyota Noah, T 241 DVU Mercdes Benz, T 751 DKC Toyota Racts na T 974 DMR Toyota Brevis.
Katika tukio jingine jeshi hilo, limewakamata watu wanne kwa tuhuma za kutenda makosa ya unyang’anyi wa kutumia nguvu na kuiba / kupora pikipiki toka kwa waendesha pikipiki @bodaboda.
Kamanda Muliro amewataja watuhumiwa hao ni Hizza Herbert (52), Mkazi Tabata, Richard George (45), Mkazi wa Buguruni, Arif Henry (21), Mkazi wa Buguruni na Saad Mohamed (25), Mkazi wa Mburahati.
“Watuhumiwa hawa walikamatwa na vielelezo Pikipiki nne walizozipora maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam, ambazo ni MC 414 CJX, MC 524 CUH, MC 731 CWE na MC 754 CQK. Baadhi ya pikipiki hizo zimeshatambuliwa na wamiliki halali,”amesema.
Soma zaidi: Watatu kizimbani madai ya kusafirisha dawa za kulevya
Ameongeza kuwa watuhumiwa wote watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili
0 Comments