CCM YAWATAKA VIONGOZI , WATENDAJI WA CHAMA NA SERIKALI KUSHUGHULIKIA CHANGAMOTO ZA WANANCHI

 KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi( CCM) Taifa Itikadi na Uenezi Shaka Hamdu Shaka amewaeleza viongozi na watendaji wote ndani ya Chama na Serikali kushughulika na changamoto za wananchi badala ya kukaa ofisini.


Shaka ameyasema hayo  akiwa ziarani  wilayani Nachingwea mkoani  Lindi.

Pamoja na mambo mengine ziara hiyo imelenga kuhamasisha na kuimarisha uhai wa chama kuanzia ngazi ya shina, kuhimiza mahusiano ndani ya chama pamoja na serikali.

Shaka ameendelea kuwahakikishia wananchi kuwa CCM na serikali vipo salama na imara katika mikono ya Mwenyekiti na Rais mahiri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

"Hii ni kwa sababu katika muda mfupi serikali anayoiongoza imetoa mwelekeo wenye matumaini makubwa ya kuimarisha ustawi wa wananchi, uchumi wa nchi yetu, kuvutia uwekezaji zaidi, kuzalisha ajira kwa vijana na kuimarisha ulinzi na usalama wa mipaka ya Nchi yetu na raia wote,"amesema Shaka

Shaka amewataka viongozi na watendaji wote ndani ya serikali kuchapakazi kwani Chama, Rais Samia na wananchi wanataka matokeo yanayoonekana na yanayopimika kutoka kwenye utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM 2020-2025.

Wakati huo huo Shaka ameilekeza Wizara ya Nishati kuhakikisha wanamaliza tatizo la kukatikakati kwa umeme linaloendelea maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Wilaya ya Nachingwea.

Shaka pia amewataka wananchi kujitokeza kushiriki kikamilifu katika zoezi la sensa ya watu na makazi itakayofanyika mwaka 2022. Alihimiza serikali inatumia gharama kubwa kukamilisha zoezi hilo kwani taarifa zake zina umuhimu mkubwa katika kusukuma maendeleo ya nchi mbele zaidi hivyo ni muhimu kila mmoja kulishiriki.

Shaka yupo kwenye ziara ya Sekretarieti ya CCM Taifa iliyopo kwenye ziara mkoani Lindi ikiongozwa na Katibu Mkuu wa CCM  Daniel Chongolo.




TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments