MADIWANI WA MANISPAA YA TABORA WAMPONGEZA RAIS SAMIA KWA HOTUBA YAKE KATIKA MKUTANO WA 76 BARAZA KUU LA UN

Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora  limempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi alivyowasilisha hotuba yake ya kwanza katika Mkutano wa 76 Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa kugusa maslahi mapana ya wananchi.

Tamko hilo limetolewa jana na Mstahiki Meya wa Manispaa ya Tabora Ramadhani Kapela kwa niaba ya Madiwani wenzake walipokuwa kwenye Baraza Maalum la Madiwani.

Alisema wao kama wawakilishi  wa wananchi kutoka Kata mbalimbali za Manispaa ya Tabora wameguswa na kuvutiwa na mambo mbalimbali yaliyomo kwenye hotuba hiyo yakiwemo Tanzania kuendelea kuwa ushirikiano wa karibu katika siasa za kimataifa.

Kapela alisema jambo linguine liliwagusa katika hotuba yake ni pamoja na suala  kuweka nguvu za pamoja katika kukabiliana na janga la maambukizi ya virusi vya UVIKO 19.

Alisema wao kama Madiwani wataendelea kumuombea kwa Mungu ili aendelee na kazi nzuri anazozifanya kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi na kuwatengenezea Watanzania mazingira ya kuwa  na afya nzuri .

Aidha Mstahiki Meya huyo aliwataka Madiwani wote kuendelea kutoa elimu kwa watu wao juu ya umuhimu wa kushiriki zoezi la kupata chanjo ya kukabiliana na jana la UVIKO 19.

Alisema kama viongozi wa Kitaifa, Mkoa na Wilaya wamechanja ni vema wananchi nao wakachanja ili kulinda nguvu kazi ya Taifa isije ikapote na kurudisha nyuma uchumi wa Manispaa ya Tabora na Taifa kwa ujumla.

Katika hatua nyingine Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora kwa kauli moja limepitisha taarifa ya ufungaji wa hesabu za Halmashauri kwa mwaka 2020/21.

Wakichangia taarifa hiyo Madiwani wamewataka wataalamu kufanyia kazi kasoro zote zilizojitokeza katika ukaguzi uliopita ili suala la kupata hati chafu lisijirudie tena.

Wakati huo huo Mkuu wa Wilaya ya Tabora Dkt. Yahya Nawanda amewataka Madiwani kusaidia kutoa elimu kwa watoto waliopo katika Kata zao kujiepusha na vitendo vya uhalifu.

Alisema kuna baadhi ya watoto ni wanafunzi hivi karibuni katika Manispaa hiyo wamekamatwa kwa tuhuma za kushiriki vitendo vya ukataji mapanga na kuwanyang’anya watu mali zao.

Dkt. Nawanda alisema kuwa mtoto hakumuondoi kwenye kosa kama atabainika kushiriki vitendo vya kiharifu.


Mstahiki Meya wa Manispaa ya Tabora Ramadhani Kapela akisoma dua jana kabla ya kuanza kwa  Baraza Maalum la Madiwani la kupitia taarifa ya ufungaji wa hesabu za Halmashauri kwa mwaka 2020/21.


Madiwani wa Manispaa ya Tabora wakiimba wimbo wa Taifa jana kabla ya kuanza kwa Baraza maalumu la kupitia taarifa ya ufungaji wa hesabu za Halmashauri kwa mwaka 2020/21
                             NA TIGANYA VINCENT

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments