SIJARIDHISHWA NA GHARAMA ZA UJENZI KITUO CHA AFYA NAIPANGA, LINDI – MAJALIWA.

 WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema hajaridhishwa na gharama zilizotumika katika upanuzi wa kituo cha Afya cha Naipanga kilichopo Wilayani Nachingwea Mkoa wa Lindi na kusema kiasi cha shilingi Milioni 600 zilizotumika katika upanuzi wa kituo hicho hakiendani na uhalisia wa majengo yaliyojengwa.


Kufuatia hatua hiyo, Waziri Mkuu ameagiza Mganga Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea Dkt. Charles Mtabho asihamishwe au kuondoka katika Wilaya hiyo hadi atakapokamilisha ujenzi wa majengo yote pamoja na baraza za kutembeza wagonjwa.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatatu Oktoba 25, 2021) wakati akikagua mradi wa upanuzi wa kituo hicho cha afya pamoja na kuzungumza na wananchi katika muendelezo wake wa ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Lindi.

Amesema Serikali imetoa muongozo katika maeneo yote yanayojengwa Vituo vya Afya kwa kiasi cha shilingi milioni 400 hadi 500 kituo kinakuwa kimekamilika kwa ujenzi wa majengo yote muhimu ikiwemo ujenzi wa chumba cha upasuaji, wodi ya wazazi, maabara, chumba cha kufulia nguo, chumba cha kuhifadhia maiti, kuchomea taka pamoja na nyumba za watumishi.

Awali akikagua Mradi wa Ujenzi wa Shule ya Sekondari Maalum ya Wavulana ya Masomo ya Sayansi Waziri Mkuu ametoa pongezi kwa wananchi wa kijiji cha Chiumbati kwa kujitolea eneo bure kwa Serikali ili kuwezesha ujenzi wa shule hiyo.

“Nawapongeza sana wananchi wenzangu kwa uzalendo mkubwa mliouonesha kwa Nchi yenu, kitendo hiki ni cha kuigwa na namna mnavyoendelea kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya sita katika kusogeza na kuboresha huduma kwa wananchi.

Awali, akitoa taarifa ya Utekelezaji wa ujenzi huo Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Nachingwea Eng. Chionda Kawawa amesema mradi huo unatekelezwa kwa Ushirikiano wa michango ya wananchi, fedha kutoka Serikali kuu pamoja na Mapato ya ndani ya Halmashauri na awamu ya kwanza itagharimu Shilingi Milioni 556.

Mradi huo hadi kukamilika kwake unatarajiwa kuwa na Madarasa 32, Nyumba za walimu 20, maabara za kemia, fizikia, baiolojia, mabweni 20 utaweza kuwahudumia wanafunzi 1600, kwa mgawanyo wa wanafunzi 800 kidato cha kwanza hadi cha nne na 800 wa kidato cha tano na sita mtawalia


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akikagua maendeleo ya ujenzi wa wodi daraja la kwanza katika Hospitali ya Halmshauri ya Wilaya ya Nachingwea, Oktoba 25, 2021 (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akimsikiliza Dk. Ramadan Maiga (kukhoto)Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya wilaya ya Nachingwea wakati alipokagua maendeleo ya ujenzi wa wodi daraja la kwanza katika Hospitali hospitali hiyo, Oktoba 25, 2021 (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Baadhi ya Madiwani, Watumishi na wananchi wa Halmaahauri ya Wilaya ya Nachingwea wakimsikiliza Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, wakati alipozungumza nao kwenye ukumbi wa Chuo cha Ualimu Nachingwea Oktoba 25,2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

 

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na Madiwani, watumishi wa Umma na wannachi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea Katika ukumbi wa Chuo cha Ualimu Nachingwea, Oktoba 25, 2021 (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments