Mkuu wa Mashtaka wa serikali ya Tunisia ameamua kuwasilisha mahakamani kesi dhidi ya Rachid al-Ghannouchi, kiongozi wa harakati ya Kiislamu ya An-Nahdhah, ambaye ni Spika wa bunge lililovunjwa pamoja na aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiyo Youssef Chahed.
Nabil al-Qarawi, ambaye ni kiongozi wa chama Qalb Tunes na baadhi ya wanaharakati wa kisiasa, akiwemo Salim Ar-Riyahi na Abdulkarim Az-Zubayd wameuanganishwa pamoja na Ghannouchi na Chahed katika kesi hiyo iliyofunguliwa katika mahakama ya mwanzo ya Tunisia.
Wote hao wanatazamiwa kufunguliwa mashtaka yakiwemo ya kuvunja sheria za kampeni za kisiasa, kutobainika wazi vyanzo vyao vya mapato ya fedha za kampeni na makosa mengine yanayohusiana na sheria ya uchaguzi ya nchi hiyo.
Mkuu wa Mashtaka wa Serikali ya Tunisia amesema, uamuzi wa kuwafungulia mashtaka wanasiasa hao umetokana na ripoti ya idara ya ukaguzi wa hesabu kuhusu uchaguzi wa mapema wa rais uliofanyika mwaka 2019.
Tangu mwishoni mwa mwezi Julai mwaka jana, Tunisia imegubikwa na mgogoro wa kisiasa uliosababishwa na hali mbaya ya uchumi na matatizo yaliyotokana na hatua ya kukabiliana na virusi vya corona.
Mnamo wakati huo na katika hatua ambayo haikutarajiwa, Rais Kais Saeid wa nchi hiyo alimuuzulu waziri mkuu na kusimamisha shughuli za bunge na kushika hatamu zote za uendeshaji nchi.../
0 Comments