Serikali Yaomba Vyombo Vya Habari Kuelimisha Kuhusu Anwani Za Makazi

 


Serikali imeviomba Vyombo vya Habari nchini kuendelea kuelimisha jamii kuhusu Mfumo wa Anwani za Makazi ikiwemo matumizi na utunzaji wa miundombinu ya mifumo hiyo.

Hayo yamesemwa leo mkoani Katavi na Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Kundo Mathew wakati wa ziara yake ya kukagua na kuhamasisha utekelezaji wa Operesheni ya Anwani za Makazi ambapo amesema kuwa Vyombo vya Habari vina mchango mkubwa katika kuelimisha Watanzania kuhusu Mfumo huo wa Anwani za Makazi na matumizi yake.

“Serikali inaviomba sana Vyombo vya Habari nchini kuendelee kusaidia kuelimisha Watanzania kuhusu matumizi na utunzaji wa mifumo hii muhimu kwa sababu tumetumia fedha nyingi lakini pia lengo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia suluhu Hassan la kufikisha kwa wananchi huduma za maji, dharula, afya na mafanikio yake ni mafaniko ya zoezi linalokuja la Sensa ya Watu na Makazi ambalo linalenga kujua idadi ya watu na kutoa huduma kulingana na mahitaji”

Aliongeza kuwa Serikali itachukua hatua kwa wale wote watakaopotosha kuhusu zoezi la Anwani za Makazi kwa kutoa taarifa zisizo na ukweli kwa wananchi ikiwemo kuwaeleza kuwa namba hizo katika majengo yao zitatumika kuwatoza kodi.

Wakati huo huo, Naibu Waziri Kundo ameitaka Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) kuhakikisha wanatekeleza maelekezo ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa aliyoyatoa mwezi Machi mwaka huu yakuitaka TARURA kuweka nguzo katika barabara zote wanazozisimamia.

“Taasisi zote za Umma na Binafsi, zishiriki kujiwekea miundombinu ya Mfumo katika maeneo ya ofisi zao ama maeneo yao ya uwekezaji kote nchini. Vilevile, kwa Upande TARURA na TANROAD wameelekezwa kusimika nguzo zenye majina ya barabara au mitaa wanayoihudumia” Alisisitiza Naibu Waziri Kundo.

Na Immaculate Makilika 

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments