AngloGold Ashanti Yaahidi Kuendelea Kuwekeza Zaidi Tanzania.

 Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya AngloGold Ashanti, Dk. Alberto Calderon juzi amekutana na Rais Samia Suluhu Hassan na kumpatia taarifa kuhusu mwenendo wa uwekezaji wa kampuni hiyo kupitia Kampuni ya Geita Gold Mine Limited (GGML) inayojishughulisha na uchimbaji wa madini nchini.


Pia alimhakikishia Rais Samia kuwa vipaumbele vya GGML ni vya muda mrefu hapa nchini na ni uwekezaji wenye faida kwa kampuni hiyo na Tanzania kwa ujumla.

“Tumepata heshima kubwa kukutana na Rais Samia na kumuelezea vipaumbele vyetu vya uwekezaji.

“Tunatarajia kuendelea kutekeleza dhamira yetu kwa mkoa wa Geita kwa kufanya uwekezaji mkubwa kudhihirisha kuwa tupo kwa muda mrefu hapa Tanzania hasa ikizingatiwa hii ni nchi ambayo imeendelea kuudhihirishia ulimwengu kuwa ni kitovu cha uchimbaji na utafutaji wa madini," alisema

Alisema Mgodi wa Dhahabu wa Geita upo katika ukanda wa machimbo ya dhahabu kanda ya Ziwa Victoria mkoani Mwanza. Hili mojawapo eneo linaloongoza kwa uchimbaji wa dhahabu duniani.

GGML ni eneo muhimu la uwekezaji kwa AngloGold Ashanti kwani mwaka jana ilipokea kiasi cha Dola za Marekani milioni 135 kama mtaji wa uwekezaji na gharama za utafiti, pia mwaka huu imepokea kiasi cha Dola za Marekani milioni 169 kwa lengo la kupanua zaidi huduma za uzalishaji na kuboresha miundombinu yake nchini.

Uwekezaji huo umewezesha uendelezaji wa migodi mitatu mipya ya uchimbaji wa chini kwa chini ambayo ni Nyankanga, Star & Comet na Geita Hill, pia umeleta mafanikio makubwa katika ugunduzi wa mgodi mkubwa na unaokua wa Nyamulilima, ambao kwa sasa umeanza uzalishaji.

Shughuli za uchimbaji madini sasa zinakua kwa kasi hasa katika uchimbaji wa dhahabu kwani hadi sasa kuna wakia milioni nane (8.3Moz) za dhahabu na mwamba wenye mashapo ya madini mbalimbali wenye wakia zaidi ya milioni mbili (2.65Moz).

Shughuli hizi za uchimbaji wa dhahabu GGML zimeajiri karibia wafanyakazi 6,000 wa kudumu na wakandarasi.

Pia GGML ndio mgodi salama zaidi katika migodi yote inayomilikiwa na AngloGold Ashanti hasa ikizingatiwa hadi sasa hakuna taarifa za majeraha kwa karibia miaka mitano iliyopita.

Aidha, tangu GGML ianze uzalishaji zaidi ya miaka 20 iliyopita, mgodi umelipa kodi na mirabaha zaidi ya Dola za Marekani bilioni 1.9 kwa Serikali ya Tanzania na kutoa ajira kwa maelfu ya watu wanaozunguka mgodi huo.

Hivi sasa, asilimia 98 wafanyakazi wa mgodi ni Watanzania na asilimia 82 ya uongozi wa kampuni ni Watanzania vilevile.

Mgodi wa Dhahabu wa Geita pia unasalia kuwa miongoni mwa walipakodi wakubwa Tanzania, nafasi ambayo kampuni hii imeshikilia kwa miaka kadhaa ambapo jumla dola za Marekani milioni 242 zimelipwa mwaka jana kwa Serikali.

Pia GGML ni mojawapo ya wawekezaji wakubwa kwenye Mpango wa Uwajibika wa Kampuni kwa Jamii (CSR) kwani kwa mwaka jana mgodi uligharamia miradi mbalimbali yenye thamani ya dola za Marekani milioni 6.1.

“Tunashukuru kwa msaada tunaoendelea kuupata kutoka kwa serikali ya Tanzania na tunajivunia mchango wetu kwa jamii zinazotupokea kupitia uwekezaji wa miradi mbalimbali ya kijamii, elimu, kilimo, afya, miundombinu na maendeleo ya kiuchumi.

“Tumejitolea kuhakikisha Geita inabaki kuwa mgodi mzuri na wenye faida kwa muda mrefu ambao unaweza kuleta manufaa ya kudumu kwa wadau wake wengi nchini Tanzania," alisema Dk. Calderon.

Rais Samia Suluhu Hassan, akiwa katika picha ya pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya AngloGold Ashanti Dk. Alberto Calderon mara baada ya mazungumzo yao Ikulu Chamwino Jijini Dodoma tarehe 23 Mei, 2022.

Rais Samia Suluhu Hassan, akizungumza na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya AngloGold Ashanti Dkt. Alberto Calderon mara baada ya kuwasili Ikulu Chamwino Jijini Dodoma tarehe 23 Mei, 2022. 

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments