Utata wabunge 19 kuitwa Baraza Kuu Chadema


 Wakati Chadema ikithibitisha kuwaita wabunge 19 wa viti maalumu waliofukuzwa uanachama kuhudhuria katika kikao cha Baraza Kuu kitakachoanza Mei 11, baadhi wamesema barua walizopewa hazielezi kuhusu rufaa walizokata.

Wabunge hao wakiongozwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha), Halima Mdee walifukuzwa uanachama na kamati kuu ya chama hicho, Novemba 2020 baada ya kwenda kuapishwa kuwa wabunge wa viti maalumu bila kuwa na baraka za chama.

Hata hivyo, waliandika barua za kukata rufaa, huku wakisisitiza kuwa bado ni wanachama.

Wabunge wengine ni Grace Tendega, Esther Matiko, Cecilia Pareso, Esther Bulaya, Jesca Kishoa, Hawa Mwaifunga, Tunza Malapo, Naghenjwa Kaboyoka, Sophia Mwakagenda, Kunti Majala, Anatropia Theonest, Salome Makamba na Conchesta Rwamlaza.

Wengine ni Agnesta Kaiza, Nusrat Hanje, Asia Mohamed, Felister Njau na Stela Fiyao.

Akizungumza juzi na Mwananchi kupitia mtandao wa WhatsApp, Katibu Mkuu wa Chadema, John Manyika alisema maandalizi ya Baraza Kuu yanaenda vizuri.

“Tumewaandikia barua za mwaliko kuja kusikiliza rufaa zao,” alisema Mnyika.

Alieleza kuwa, mialiko imeshapelekwa kwa wajumbe na wahusika wote, hivyo Baraza Kuu litafanyika Mei 11 mwaka huu jijini Dar es Salaam kama ilivyopangwa.

Alizitaja ajenda zitakazojadiliwa kuwa ni mpango mkakati wa miaka mitano ya chama, mpango kazi wa mwaka wa chama na mikakati ya kukiimarisha chama itajadiliwa na kupitishwa.

Hata hivyo, akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, mmoja wa wabunge hao, Sophia alisema barua walizopewa ni kwa ajili ya kuhudhuria Baraza Kuu kama wajumbe.

“Wao si waliwaambia ninyi kuwa tumefukuzwa? Lakini leo sisi tumeitwa kwenye chama chetu tunakwenda. Ni chama chetu ndiyo maana tunakwenda na ndiyo maana wametutumia barua yenye nembo,” alisema.

Alipoulizwa kuhusu utetezi walionao kwa rufaa walizokata alisema: “Hapana, wewe andika wanachama 19 wamealikwa Baraza Kuu.” Alisema kwa muda mrefu tangu wafukuzwe uanachama waliitwa kuwa ni ‘wanachama wa Spika’ wa zamani wa Bunge, Job Ndugai au wa Spika wa Bunge Dk Tulia Ackson.

“Ndiyo maana nimealikwa kwa sababu huwezi kwenda kikao cha CCM kama wewe siyo CCM. Sisi tangu day one (siku ya kwanza) tuliandika rufaa, sasa tumeitwa.”

Naye Kunti Yusufu aliunga mkono kauli hiyo akisema; “Mimi sijaitwa Baraza Kuu kwa ajili ya kujitetea, nimeitwa kama mjumbe wa kikao.”

Alipoulizwa kuhusu kufukuzwa uanachama, alisema, “Mimi sijafukuzwa, kikao cha Baraza Kuu kinapoitwa wanaoalikwa ni wanachama na wajumbe wa kikao, sasa mtu aliyefukuzwa anaalikwaje kwenye kikao?” alihoji.

“Barua yangu ya mwaliko imeandikwa kuhudhuria kikao, siyo ya kukata rufaa. Uanachama wetu uko vizuri wala haujawahi kuwa na shida.”

Jana, Mnyika alipotafutwa kuzungumzia utata huo, alisema hawezi kujibu kwa kuwa alikuwa kwenye kikao.


Wachambuzi

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Mwananchi, baadhi ya wachambuzi wa siasa wameonesha uwezekano mdogo wa wabunge hao 19 kurejeshwa Chadema.

Mchambuzi wa masuala ya siasa, Dk Faraja Kristomas alisema uamuzi wa kuwafuta uanachama wanasiasa hao 19 utakuwa na faida zaidi kwa Chadema kuliko hasara. “Kwanza kabisa itaonesha chama kimedhamiria kuponya mpasuko ulioibuka miongoni mwa wanawake wa Chadema kupitia Bawacha.”

Alisema mpasuko huo ulitokana na namna wabunge hao walivyopatikana na kusababisha baadhi ya wanawake kukosa imani na viongozi wa kitaifa, wakidhani walibariki kisirisiri mchakato huo.

Kwa upande wa hasara, alisema chama kitakosa michango ya namna mbalimbali kutoka kwa wanasiasa hao, katika ujenzi wa taasisi.

Tofauti na mtazamo huo, mchambuzi wa masuala ya siasa, Dk Onesmo Kyauke alisema kufanyika mazungumzo yatakayowarudisha katika mstari wa chama wanasiasa hao ni tija zaidi kwa Chadema kuliko kuwafukuza.

Kwa upande mwingine, Dk Kyauke alisema kurudishwa kundini ni hatari kwa chama hicho kwa kuwa tayari wanatambulika kwa uasi walioufanya.

“Ni watu walioasi, kuwarudisha bungeni ni kama hawatakuwa kwa masilahi ya Chadema kwa sababu ni waasi,” alisema.

Imeandikwa na Elias Msuya, Bakari Kiango na Juma Issihaka.

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments