Maridhiano ya Kitaifa katika dhana ya Demokrasia nchini, ni dhamira njema ya Rais Samia kwa Taifa letu

 Maridhiano ni hatua inayofikiwa kwa dhana ya kuleta makubaliano ya pamoja kwa jambo lenye masilahi kwa makundi mawili au zaidi yenye mtazamo au itikadi tofauti katika nchi husika.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiongoza Kikao cha majadiliano pamoja na Viongozi Wakuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Ikulu Chamwino Jijini Dodoma tarehe 20 Mei, 2022. Baadhi ya Viongozi wa CHADEMA waliohudhuria Kikao hicho walikuwa ni Mwenyekiti Freeman Mbowe, Makamu Mwenyekiti Zanzibar Saidi Issa Mohamed, Katibu Mkuu wa Chama hicho, John Mnyika pamoja na baadhi ya Wajumbe wa Kamati Kuu na Sekretarieti ya Chama hicho.

Inapotokea makundi haya hayakubaliani katika mizingira baadhi ya mambo, basi kwa taifa lenye wastaarabu wanakubalina kukutana meza moja kuzungumza namna ya kwenda ili kujikwamua katika hali ya kutoelewana na mambo haya huwa ni muhimu sana kufanyika wakati wa amani.

Inapobainika kama kuna jambo la namna hiyo kwa pande zote au upande mmoja basi kundi moja huleta hoja ya Maridhiano kwa lengo la kutimiza MALENGO Mahususi yaliyotarajiwa kwa makundi yote mawili na kuona kuna umuhimu wakukaa pamoja ili kuzungumza.

Mwaka 2007 nchi ya Kenya ilipitia katika wakati mgumu sana katika mchakato mzima wa Uchaguzi Mkuu, jambo ambalo lilifanya kuzaliwa kwa Maridhiano ya Kitaifa kwa kuyakutanisha makundi yote kinzani.

Maridhiano hayo yakawa ni baada ya kutokea mauaji ya baadhi ya watu na kufanya nchi hiyo kupoteza nguvu kazi ya taifa kutokana na zoezi zima la uchaguzi mkuu huo kutawaliwa na sintofahamu na kufanya uwepo wa vurugu na kusababisha viongozi wa kitaifa kupelekwa katika mahakama za kimataifa, kwa lengo la utetezi wa haki za binadamu.
Nchini kwetu Tanzania suala la maridhiano limejitokeza katika vipindi mbalmbali vilivyopita na mpaka sasa RAIS WETU ameendelea kujenga msingi uliyojengwa na waasisi wa Taifa Letu.

Sote tunajua uundwaaji wa Serikali ya Umoja wa kitaifa katika Serikali ya Zanzibar ni matokeo ya maridhiano hayo ambayo yalitokana na mnyukano wa kisiasa kati ya chama tawala na vyama vya upinzani wakati huo chama chenye nguvu Tanzania Zanzibar kikiwa ni chama cha wananchi CUF.

Ni dhahiri maridhiano yana nguvu kubwa duniani, kwani ukitazama kwa mawanda mapana kwa sasa namna siasa za Zanzibar zinavyoleta na kuliweka taifa hilo pamoja, kujenga Mshikamano, Upendo na Umoja wa kitaifa kwa Wazanzibar inafanya nchi hiyo kuwa na utulivu mkubwa na kufanya upatikanaji wa maendeleo ya haraka katika nchi.

Uwepo wa maridhiano kwa baadhi za nchi katika Afrika unatokana na mambo yafuatayo: - Mosi, Uzalendo wa kiongozi Mkuu wa nchi, unafanya uwepo wa Maridhiano jambo ambalo linaongozwa na Dhamira Njema kwa kiongozi huyo.
Pili,Utashi wa kisiasa wa kiongozi wa Mkuu wa nchi huchochea uwepo wa maridhiano katika Taifa husika jambo ambalo huleta Umoja wa kitaifa.

Tatu, Uimara wa chama kinachotawala Taifa husika kwani, nidhahiri sote tunajua katika Bara la Afrika vipo Vyama Vya Siasa vimefanya kazi kubwa ya harakati zauhuru na ukombozi katika nchi zetu za Afrika hasa kusini mwa Afrika, lakini leo vimepotea yote haya ni Udhaifu mkubwa wa kukosa uimara katika kujenga Maridhiano katika nchi zao.

Tazama KANU nchini Kenya na nchi nyinginezo, tazama nchi ya Libya ambayo pia ilikumbwa na athari ya kukosekana kwa uimara wachama tawala hadi sasa taifa hili lipo kwenye mateso makubwa ya janga la vita yawenyewe kwa wenyewe.

Dhana ya uimarishaji wa demokrasia na maridhiano katika nchi inaleta matokeo chanya katika Maendeleo, Uimarishaji wa Uchumi wake wa ndani, kujenga twasira nzuri ya Taifa katika anga za kimataifa jambo hili huleta na kuimarisha diplomasia za kimataifa pia.

Ushauri wangu kwa Vyama Vya Siasa kikiwemo chama Chetu Tawala

Mosi, Ni vema Vyama vyote vya siasa kuunga na kukubaliana na jitihada na Dhamira Njema ya RAIS WETU ya kuanzisha siasa za maridhiano kama taifa bila kubeba Ukinzani wa kisiasa kwani kwa kufanya hivyo nchini itaimarika zaidi nakutunza Utaifa wetu.
Pili, Vyama Vya Siasa vibebe Uzalendo Mkubwa kwa Taifa letu na kuachana namasilahi binafsi ya Vyama vyao ili RAIS WETU aweze kutimiza ndoto yake ya kujenga Nchi yenye Maendeleo Imara zaidi.

Tatu, Vyama vya siasa vina wajibika kutunza Amani yetu kwa kila kimojawapo kuridhia uwepo wa Maridhiano katika Nchi,kwani kwa kufanya hivyo dhamira njema ya Rais Wetu itakua na tija kwamaendeleo ya taifa letu.

Nne, Maridhiano yatasaidia kujenga Umoja na Mshikamano ndani na nje ya Vyama vyetu vya Siasa.

Tano, uwepo wa maridhiano katika nchi utasaidia taifa kupanga na kufikia Malengo yake mahususi ya kuleta maendeleo kwa watu wake hasa katika nyanjambalimbali kama vile masuala ya kiuchumi na shughuli zingine za kijamii.

Ni dhahiri kuwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan ameamua kujenga Taifa imara lenye upendo, Mshikamano, Umoja, Amani na Utulivu kwa watu wake.

Sote tuna kila sababu ya kukubali maridhiano kwa afya ya Taifa letu, tuipende nchi yetukuliko tofauti za vyama vyetu vya siasa kwani nchi ni zaidi ya vyama.

Dhamira Njema ya RAIS WETU ni kuleta siasa safi na yenye tija kwa maendeleo ya nchi, hivyo Watanzania wote tuna kila sababu ya kukubali maridhiano haya ili tuweze kufanya maendeleo endelevu kwa pamoja.

Mwandishi;
Mwalimu Meijo Laizer ni,
Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Mstaafu
Wilaya ya Siha
0755898037

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments