TOBIKO MAKOLO AWASHUKIA VIKALI WAPOTOSHAJI MBELE YA WAZIRI MKUU,AFURAHIA MAISHA MAPYA YA MSOMERA,HANDENI TANGA

Mbele ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa  mwananchi mpya wa kijiji cha msomera aliyehamia kwa hiyari kutoka Ngorongoro Richard Sali Tobiko Ole Mokolo ametoa ushuhuda wa wananchi hao kupewa upendeleo ambao hawakuutarajia kamwe kuupata kutoka kwa serikali na kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa upendo wake kwao aliouoneesha.


Ushuhuda huo, ulitolewa na mwananchi huyo ni pamoja na sasa kumiliki ardhi yenye jina lake na mkewe, ambapo hakuwahi kuiona au kuifahamu hati, kupewa nyumba yenye vyumba vitatu na sebure ikiwa katika eneo lenye ukubwa wa ekari mbili na nusu, kupewa shamba lenye ukubwa wa ekari tano, kupatiwa miundombinu yote ya huduma muhimu za jamii ikiwemo maji safi salama na ya uhakika, umeme, uangalizi wa wataalumu wa mifugo na madaktari wa kibinadamu.

Vitu hivyo, amevitaja kama moja ya mambo makubwa ya upendeleo waliofanyiwa watu hao waliohama kwa hiyari kutoka Ngorongoro na ametumia nafasi hiyo kumuomba Waziri Mkuu Majaliwa kuendelea kutoa elimu sahihi juu ya eneo hilo kwa kuwa kuna upotoshaji mkubwa unaofanyika kuwazuia watu wanaotaka kuhama kwa hiyari kuja Msomera

Akizungumza mbele ya Waziri Mkuu, Majaliwa, mwananchi huyo bwana Ole Mokolo ambaye tayari amechangamkia fursa kwa kubadilisha moja ya chumba chake kuwa duka la bidhaa mbalimbali kuwauzia wananchi wenzake, alisema maisha ya eneo hilo ni salama na wameyapenda ndani ya muda mfupi kutokana na uwepo wa huduma zote muhimu za kijamii.

''Kwa kweli najisikia vizuri sana, mwanzo hatukujua kama itakuwa hivi, kwa fidia tulishapewa, tulipewa nyumba yenye eka mbili na mashamba eka tano, hali ya hewa ni nzuri na watoto hawaisumbui. Tunaishukuru sana serikali, Rais Samia na wewe pia Waziri Mkuu kwa kuwa nasi toka mwanzo na mama mmoja hivi simjui vizuri anatoka Mamlaka ya Ngorongoro anaitwa Joyce''.

Aliongeza ''Kwa kweli niwashauri sana wenzetu ambao wamebaki kule, wakati tunaondoka walikuwa wanatulilia ni kama tunapotea, lakini tumefika huku tunasikitikika, tunawalilia wao kwa sababu bado hawajajua hatima yao.

Akizungumzia upotoshaji unaofanywa na wanaharakati, Ole Mokolo alisema ''Nikuambie tu Waziri Mkuu kwamba kuna upotoshaji mwingi sana, tulipokuja huku tumepiga simu wengine wanasema katika group la kwanza tulilokuja tayari kuna watu tayari watatu wamegongwa na nyoka wamefariki na kuna ngombe wameliwa na wanyama wakali na wengine wamesema ngombe zangu zilifika makuyuni zimekufa, lakini ngombe wangu wazima wote wale pale na mbuzi wangu pia wapo pale''.

Aidha, alipoulizwa na Waziri Mkuu kuhusiana na upatikanaji wa maji safi na salama, mwananchi huyo alisema kuna maji mengi ambapo kuna vituo vya maji kila baada ya mita 400, kuna maji mazuri na hata mifugo haipati shida ya kunywa maji kwa kuwa muda wote wanapata majisafi na salama tofauti na Ngorongoro.

''Kule Ngorongoro ilikuwa mifugo tukinywesha maji leo, kesho hatunyweshi kwa sababu hakuna maji lakini huku maji ni mengi, tunachagua tunyeshwe ya bombani au ya kwenye visimani, sasa tumepata uhuru na haki na maisha yetu na kufanya lolote bila bughuza katika ardhi yetu'' alisema.

Akituma salamu kwa Rais Samia, Ole Mokolo alisema 'Kwanza nasema kwa majina naitwa Richard Sali Tobiko Ole Mokolo nipeleke sana salamu zangu kwa mheshimiwa rais wa jamuhuri ya muungano wa Tanznaia, mama yetu samia suluhu hassan, nimuombe sana zoezi hili angalau hata likiwa limeendaenda na yeye aje tutoe shukrani zetu kwake. tunashukurani nyingi sana za kumpa, kwa kweli ni upendeleo wa kutosha, niseme ni upendeleo wa kutosha kwa sababu sidhani kama kwa fidia tulizopata sidhani kwa fidia ambayo mtu amepata angelalamika hata kama asingepewa hivi vitu.(Nyumba, Shamba na maeneo ya malisho na kusafirisha wao, mifugo na mizigo yao). Tunamuomba Rais Samia aje Msomera, tunampenda sana na kura zetu hazina mashaka kwake''.

Juni 23, mwaka huu 2022, Waziri Mkuu Majaliwa alifanya ziara ya siku moja mkoa wa Arusha katika wilaya ya Ngorongoro na kuwaaga wananchi wanaohama kwa hiyari kutoka ndani ya hifadhi ya Ngorongoro na kuhamia Msomera kundi la watu 117 lenye kaya 27 ikiwa ni awamu ya pili ya wananchi wanaohamia katika kijiji hicho, aidha Waziri Mkuu pia alitembelea Loliondo kushuhudia eneo la kilometa za mraba 1500 linalowekewa vigingi.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimsikiliza, Bw. Richard  Tobiko Ole Makoro  (kulia) ambaye ni mmoja wa wakazi wapya wa kijiji cha Msomera wilayani Handeni Mkoa wa Tanga waliohamia katika kijiji hicho kutoka Ngorongoro wakati alipofika nyumbani  kwa  mkazi huyo kujionea  mazingira anayoishi, Juni 23, 2022

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments