Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhandisi Paskas Mragili, akifungua jana mafunzo ya siku tano ya uongozi na utawala katika michezo kwa viongozi 30 wa vyama vya michezo, vilabu na walimu kutoka wilaya zote za Mkoa wa Singida. Kushoto ni Makamu wa Rais Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau na kulia ni Afisa Michezo Mkoa wa Singida, Amani Mwaipaja..
Makamu wa Rais Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau, akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo. |
Na Dotto Mwaibale, Singida
KAMATI ya Olimpiki Tanzania (TOC) imetoa mafunzo ya siku tano ya uongozi na utawala katika michezo kwa viongozi 30 wa vyama vya michezo, vilabu na walimu kutoka wilaya zote za mkoa wa Singida mafunzo yaliombwa na Mbunge wa Singida Mjini Mussa Sima kwa lengo la kuinua michezo mkoani hapa ambayo yanatarajiwa kufikia tamati kesho kutwa Oktoba, 28, 2022.
Akifungua mafunzo hayo jana yanayoendelea Ukumbi wa Maktaba wa Shule ya Sekondari Mwenge iliyopo mjini hapa , Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhandisi Paskas Mragili, ambaye alikuwa mgeni rasmi aliwaambia washiriki kuwa mara watakapo hitimu wasiviweke kabatini vyeti vyao na kusubiri kuvitumia kugombea uongozi badala yake wakasaidie kuinua michezo na kuunga mkono jitihada za Serikali ambayo inatoa mchango mkubwa kwenye michezo nchini.
Aidha Muragili alisema Tanzania katika sekta ya michezo ipo juu na ina watu wazuri lakini changamoto iliyopo wakipelekwa kwenye uongozi wanafanya vibaya hivyo kuifanya nchi kutofanya vizuri kwenye michezo mbalimbali hususani ya kimataifa.
Alisema mafunzo hayo yanayoendeshwa na Kamati ya Olimpiki Tanzania yawe chachu kwa kuweka mipango mikakati ya kuinua michezo Singida na nchini kwa ujumla kwani sekta hiyo ni muhimu sana kwa kuwa inaitangaza Tanzania kimataifa.
Makamu wa Rais Kamati ya Olimpiki Tanzania, Henry Tandau, alisema mafunzo haya ni ya ngazi ya awali ambapo washiriki watafundishwa historia ya olimpiki, namna gani michezo inaweza kuchangia maendeleo ya mileniamu, namna ya kutengeneza mipango mikakati, umuhimu wa vyombo vya habari katika michezo.
Pia Tandau ambaye ni mkufunzi wa mafunzo hayo alisema washiriki pia watafundishwa soko la michezo na rasilimali watu katika michezo.
Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Netball Mkoa wa Singida, Farida Omari akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo alisema watazingatia kila watakachofundishwa ili watakitoka hapo wawe wameiva kwa ajili ya kwenda kuinua michezo kwenye maeneo yao.
0 Comments