Kauli hiyo inakuja baada ya Dk Bashiru kuhutubia mkutano wa Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (Mviwata) uliofanyika juzi mkoani Morogoro, huku akisema mtandao huo si chombo cha kutoa shukrani kwa yeyote yule, bali ni chombo cha kudai haki na heshima.
Alisema mtandao huo sio chombo kidogo na kuwataka wanachama wake kuulinda na kuurithisha kwa vizazi vingine kimsimamo, na kwamba wakifikia hatua hiyo, hata changamoto wanazozizungumzia zitapungua.
“(Mviwata) si chombo cha kusifu, si chombo cha kushukuru, tunakushukuru kwa fedha hizi, tunakushukuru kwa kazi hizi, mkianza kazi ya kushukuru kwa haki yenu, hamna maana,” alisema Dk Bashiru ambaye ni mbunge wa kuteuliwa na Rais.
Akizungumza juzi jijini Dodoma, Katibu Mkuu wa UVCCM, Kenani Kihongosi alisema Dk Bashiru alizungumzia maneno ambayo si ya kiungwana na yamejaa ukakasi na yamelenga kwenda kuichonganisha Serikali na wananchi hasa wakulima.
Alisema ileweke kuwa Serikali ya awamu ya sita imefanya kazi kubwa inayoenda kuacha alaDsma kwa Watanzania ikiwemo kuweka ruzuku katika mbolea ili kupunguza bei ya pembejeo hiyo nchini.
Alisema pia Serikali imetoa vitendea kazi, pikipiki, vipima udongo na kuongeza bajeti ya sekta ya kilimo, lengo likiwa ni kusaidia kukuza uchumi hasa katika sekta ya kilimo nchini.
“Sasa inapotokea kiongozi ambaye ana dhamana kubwa anatoa maneno yenye ukakasi na kusema viongozi hawapaswi kupongezwa bali wanapaswa kutolewa matamshi ya kuwashinikiza ili waweze kuwatendea wakulima, hiyo siyo sawa,”alisema Kihongosi.
0 Comments