Dk Tulia Akerwa Wakulima Kuzungushwa Kupata Mbolea, atoa Maagizo

Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson ameagiza mawakala waliopewa zabuni na Serikali  kugawa mbolea za ruzuku kwa wakulima kuzitoa na kuachana na sababu ikiwepo mifumo ya kuingiza taarifa.

Dk Tulia ametoa agizo hilo leo Alhamisi, Desemba 29, 2022 mara baada ya kupata malalamiko  ya wakulima kuhusiana na kukosekana kwa mbolea  na  kulazimika kufanya ziara ya kushtukiza kwa baadhi ya mawakala ikiwepo Kampuni ya DRTC.

“Nimefika hapa kwa suala moja tu la mbolea, maana nimepata malalamiko ya wakulima kuwa mbolea hakuna na hapa nimefika kwa wakala wa kampuni ya DRTC ipo tena ya kutosha nahitaji wakulima wapatiwe,” amesema.

Dk Tulia ambaye pia ni mbunge wa Mbeya Mjini amesema kitendo cha wakulima wadogo kukosa mbolea huku wakubwa wakinufaika sio malengo ya Serikali.

“Serikali imetoa utaratibu wa ugawaji wa mbolea kwa wakulima, sasa nashangaa ninapo elezwa mbolea hakuna na wakulima wakiangaika hali ambayo sio busara, sasa suala la mifumo ambayo wakala unalalamikia nawasilisha serikalini cha msingi wakulima kuanzia sasa wapewe mbolea,” amesema

Mkulima Faustina Charles, mkazi wa Itezi Magharibi ameiomba Serikali kuingilia kati ili waweze kupata pembejeo kulingana na mahitaji kwani msimu wa kilimo unapita bila sababu.

“Mh nimefika hapa tangu saa 12.30 za asubuhi mpaka sasa saa 7.00 mchana sijapata mbolea na tangu muda huo ndani ya saa moja wanahudumiwa watu watatu na tunapohoji tunaelezwa mbolea imekwisha tusubiri mpaka Jumanne ya Januari 3,” amesema.

Kwa upande Wakala wa Mbolea wa Kampuni ya DRTC, Leonard Mpayo alikiri kuwepo kwa changamoto na kwamba mifumo ya uingizaji wa taarifa imechangia wakulima kutopata  mbolea kwa wakati.

Wakati huo huo, Dk Tulia ameshiriki ujenzi wa vyumba sita vya madarasa kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha tano na sita katika shule ya Sekondari ya Iganzo.

Chanzo Mwananchi

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments