TANZANIA YAANZA MCHAKATO WA KUJIUNGA NA MIKATABA YA KIMATAIFA YA MAJI SHIRIKISHI

Tanzania  imeanza mchakato wa kujiunga na mikataba ya Kimataifa ya matumizi sawa na sahihi ya maji ili kuwa sanjari na watumiaji wengine wa maji hayo yanayopita katika mipaka mbalimbali Kimataifa.

Hayo yameelezwa leo (Desemba 1, 2022) na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga katika warsha iliyoshirikisha Jumuiya, Wadau mbalimbali wa Serikali na Sekta Binafsi kujadili mikataba ya Umoja wa Mataifa ya Maji Shirikishi.

Mhandisi Sanga amesema lengo la Tanzania kujiunga na mikataba hiyo ya Kimataifa ya maji shirikishi ni kuhakikisha maji yanatumika kiusawa na sahihi na kuleta faida kwa matumizi yake katika taifa la Tanzania na mataifa mbalimbali.

Hata hivyo, Mhandisi Sanga amesema Tanzania licha ya kuwa bado haijajiunga na mikataba hiyo, kwa sasa inatumia mkataba wa Kimataifa wa mwaka 1992, mkataba ambao unafanya mataifa mbalimbali kuwa na lugha moja katika matumizi ya maji shirikishi.

“Sisi Tanzania tumebahatika kuwa na vyanzo vya maji shirikishi, mfano, Ziwa Victoria na Ziwa Nyasa katika matumizi yake lazima tuangalie matumizi sahihi ili kuhakikisha na wengine wanaotumia maji hayo hawapati athari yayote”, amesema Mhandisi Sanga.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Nishati na Madini - Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Shaibu Hassan Kaduara amesema kuna umuhimu kwa taifa kuwa sehemu ya mashirikiano hayo ya mikataba ya Kimataifa ya maji shirikishi ili kutunza na kutumia maji kwa usawa.

“Kwa sisi Tanzania kuna umuhimu wa kuwa sehemu ya mashirikiano ili kutunza na kutumia maji kwa usawa, lazima tulinde maji na tutumie kwa usawa ili maji haya yasilete shida na badala yake yalete amani baina ya mataifa”, amesema Mhe. Kaduara.

Tanzania itajiunga na mikataba hiyo ya Kimataifa ya maji shirikishi baada ya vikao hivyo vya wadau mbalimbali kujadili mikataba hiyo, sanjari na kujadiliwa kwenye Vikao vya Makatibu Wakuu, Baraza la Mawaziri na Bunge kupitia na kuridhia mikataba hiyo

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga akizungumza jijini Dar es Salaam katika warsha ya iliyoshirikisha Jumuiya, Wadau mbalimbali wa Serikali na Sekta Binafsi kujadili mikataba ya Umoja wa Mataifa ya Maji Shirikishi.
Mwakilishi wa Umoja wa Ulaya akitoa hotuba yake mbele ya Wadau mbalimbali wa Serikali na Sekta Binafsi waliohudhuria warsha ya iliyoshirikisha Jumuiya, Wadau mbalimbali wa Serikali na Sekta Binafsi kujadili mikataba ya Umoja wa Mataifa ya Maji Shirikishi.
Wadau mbalimbali waliohudhuria warsha hiyo
 Chanzo Na Bakari Madjeshi, Michuzi.

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments