Hisia tofauti uteuzi wa mawaziri, Mkurugenzi wa Uchaguzi


Kufuatia mabadiliko ya baadhi ya viongozi yaliotangazwa leo Februari, 26 ambapo Rais Samia Suluhu Hassan, amewateua na kuwahamisha wizara baadhi ya  mawaziri na naibu mawaziri, wakuu wa mikoa, makatibu na naibu makatibu wakuu pamoja na kumteua Mkurugenzi wa Uchaguzi wadau mbalimbali wametoa maoni yao juu ya mabadiliko hayo.

Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma wa Chama cha wananchi CUF, Mohamed Ngulangwa amesema ni jambo la Kawaida kwa Rais kuteua na kutengua na kuhusu Tume ya Uchaguzi, wenyewe kama chama cha Wananchi CUF wanasubiri Tume huru itakayosimamia Uchaguzi Mkuu na Uchaguzi wa Serikali za mitaa, vijiji na vitongoji.

Vilevile amesema mabadiliko yoyote yatakayofanyika katika muundo wa Tume ya Uchaguzi iliyopo sasa hayawezi kuwa na tija kwenye demokrasia.


Victoria Mwanziva ambaye ni mkuu wa Wilaya ya Ludewa katika maoni yake ya mtandao wa Twitter amesema anawatakia kazi njema wote viongozi wote waliochaguliwa huku akiwataka waweke mbele maslahi ya Taifa.

“Kila la Kheri viongozi wetu, tunazidi kuwaombea na kuwatakia Kheri katika utumishi wenu kwa Taifa letu, Tanzania.” Amesema Mwanziva.

Kwa upande wake Askofu William Mwamalanga ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya kitaifa ya Maaskofu na Mashekhe ya maadili, amani na haki za binadamu kwa jamii ya madhehebu ya dini nchini amesema uteuzi wa leo umetiwa doa kwa kuteuliwa  kwa Mawaziri na Manaibu ambao wizara   walizotoka hawakufanya vizuri.

“Tukichukulia kwa mfano wizara ya Ardhi, Elimu, Afya na kilimo ni muhimu kuleta sura za kazi zaidi watu wanaothubutu badala ya kuwapa watu uwaziri, ukatibu mkuu na ukuu wa mkoa kwa kisiasa, hatuwezi kuingia kwenye hatua za kweli za kimaendeleo” amesema Mwamalanga.   

Yohana Msita kutoka Twitter amewahasa viongozi hao kwa kuwataka kuchapa kazi ili kuendana na ndoto za Rais.

“Nendeni mkapambane kutimiza ndoto za Rais Samia” amesema Msita.


John Pambalu mwenyekiti wa Baraza la vijana Chadema (Bavicha) amesema bado kuna haja ya kuwa na katiba mpya kwa ajili ya kupunguza mamlaka makubwa anayopewa Rais katika kufanya uteuzi.

“Katika madai ya Katiba, moja kati ya jambo linalopigiwa kelele na wadau wote wa demokrasia na utawala bora, ni mamlaka makubwa ya Rais kuteua watu bila ya kuwa na vyombo vya kisheria vilivyopewa mamlaka ya kumbana ili achague watu ambao wamekidhi vigezo na matarajio chanya ya walio wengi,”amesema.

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments