MSIUZE ARDHI KAMA NYANYA SOKONI-MAMASITA

 Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wa CCM Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, Haiyo Yamati Mamasita, amewataka wananchi wa eneo hilo kutouza ardhi rejareja kama nyanya inavyouzwa sokoni.


Mamasita ameyasema hayo kwenye kata ya Edonyongijape katika maadhimisho ya miaka 46 ya kuzaliwa CCM ambayo kwa jumuiya ya wazazi wilaya hiyo yamefanyika kijiji cha Edonyonyijape.

Amesema kwa nafasi yake ya Mwenyekiti wa Wazazi wa Wilaya hiyo atahakikisha anasimama kidete kupinga uuzaji ardhi kiholela kwani ndiyo urithi wa jamii ya eneo hilo.

“Japokuwa hivi sasa kuna baadhi ya watu wenye tamaa ya ardhi wanachukia kwa sababu tunapinga uuzaji ardhi, hatutajali hilo kwani tunasimama kwa niaba ya wananchi,” amesema Mamasita.

Amesema mkutano mkuu wa kijiji ndiyo wenye dhamana ya kupitisha uuzaji wa ardhi ila baadhi ya viongozi wenye tamaa wanajaribu kufanya udanganyifu na kuuza ardhi kiholela.

“Wenyeviti wa vitongoji hawana mamlaka ya kuuza ardhi ya eneo hilo zaidi ya mkutano mkuu wa kijiji kupitisha hayo, hivyo wananchi kuweni makini ardhi yenu isiuzwe kiholela,” amesema Mamasita.

Amesema anampongeza Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Dkt Suleiman Hassan Serera kwa kusimama kidete katika kutetea ardhi ya wananchi isiporwe hivyo wananchi waendelee kumpa ushirikiano.

“Tunampongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kumbakiza Simanjiro Dkt Serera, vyombo vyake vimeona kwa macho makali kuwa huyu kiongozi anachama kazi ndiyo sababu akaachwa Simanjiro hivyo tumuunga mkono,” amesema Mamasita.




TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments