Zaidi ya wananchi 19, 300 wajengewa zahanati Shinyanga

Ili kusogeza huduma za Afya karibu na wananchi, Serikali imejenga zahanati iliyogharimu zaidi ya Sh104 milioni katika Kata ya Masekelo Manispaa ya Shinyanga itakayohudumia zaidi ya wananchi 19,333.

Akizindua zahanati hiyo leo Aprili 26, 2023 ikiwa ni maadhimisho ya miaka 59 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Christina Mndeme amesema wananchi hao wataondokana na adha ya kwenda  kupata matibabu nje ya kata hiyo.

“Ndugu zangu wanamasekelo kabla ya muungano tulikuwa na zahanati 10 kwa mkoa mzima, lakini kwa sasa tuna zahanati 250 hivyo tunatakiwa kuendelea kuiunga mkono Serikali ya awamu ya sita ili iweze kufanya maendeleo makubwa zaidi,”


“Zahanati hii imeletwa hapa  kwa ajili ya wananchi, hivyo niwaombe tuitunze tusilete  hujuma yeyote, pia niwaombe wananchi wote wa Mkoa wa Shinyanga muendelee kujikinga na Malaria kwani mkoa wetu bado una maambukizi ya Malaria hivyo ni jukumu langu na wewe kuchukua tahadhari kwa kutumia vyandarua tulivyopewa,”amesema Mdeme

Amesema maendeleo yote ya mkoa huo ikiwemo  zahanati ya Masekelo yanatekelezwa na ilani ya CCM hivyo huduma zote zitapatikana zikiwemo za mama na mtoto pamoja na huduma za wajawazito.

Katika hatua nyingine, Mdeme amewataka wanafunzi  mkoani humo kutoshawishika ili watimize ndoto zao za maisha.

Katibu wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Dornad Magesa amesema Chama hicho kitaendelea kusimamia ilani yake na kuhakikisha Serikali inatekeleza miradi mbalimbali ya kimaendeleo na kuwataka wananchi waendelee kukiamini.

Baadhi ya wananchi wa kata hiyo wameishukuru Serikali kwa kuwajengea zahanati hiyo wakidai walikuwa wakipata shida kwenda kutibiwa katika zahanati za kata zingine lakini kwa sasa watapata matibabu karibu.

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments