UWT yawaonya wanaochonganisha wabunge na wana CCM

Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) Mkoa wa Shinyanga imewaonya baadhi ya wanachama wa chama hicho wenye tabia ya kujipendekeza na kuchonganisha wenzao kwa wabunge wa mkoani hapo.

Akizungumza na wajumbe wa baraza la UWT mkoani Shinyanga lililofanyika katika ukumbi mdogo wa CCM leo Jumatano Julai 12, 2023, Mwenyekiti wa jumuiya hiyo mkoani humo, Grace Bizulu amewataka kuacha tabia hiyo mara moja akidai inasababisha mpasuko mkubwa ndani ya jumuiya na CCM.

Bizulu amesema  uchaguzi umeisha hivyo kila mmoja afanye majukumu yake badala ya kupigana vikumbo akitaka kila mmoja ampende mwenzake, kukisemea vizuri chama hicho, kusikiliza kero zilizopo kwenye jamii na kuzitatua kwa sababu wote ni watoto wa mama mmoja CCM.


“Imefikia wakati tunaanza kurekodiana mmezidi hiyo tabia niwaombe muache mara moja, nikimjua mtu anayechonganisha nitamwambia katibu asimualike kwenye vikao vyangu, tuweni na hofu ya Mungu, tupendane, pale tunapokosea tuambizane sio kuendekeza majungu hayajengi yanabomoa,"

“ Niwaombe ndugu zangu tuwe na upendo na mshikamano tusiwe wabomoaji wanaopenda kuvuruga na kujipendekeza, kwani watu wanaofanya hivyo wanatuharibia Mkoa wetu na kuonekana hatuna ushirikiano na umoja. Ndiyo maana tunashindwa kupata wageni wakubwa kwa sababu ya watu wachache wanaopenda kujipendekeza,” amesema Bizulu

"Sisi wanawake tunatakiwa tuwe na upendo na mshikamano,tufanye kazi kama tulivyoahidi wakati tunaomba kura kwa wananchi niombe huu wakati mniache nifanye kazi, kwa kushirikiana na wabunge wangu wote. Sitaki mambo ya ubaguzi tusibaguane kwamba huyu ni wa nani na huyu ni wanani tufanye kazi kwa pamoja, wale waomba fedha watafute njia zingine za kushawishi sio kusema uongo," ameongeza Bizulu

Mbunge  wa viti maalumu Mkoa wa Shinyanga, Santiel Kilumba amewaomba wanawake watoe ushirikiano ili  kuhakikisha wanajenga nyumba ya katibu wa UWT na ofisi ya wabunge  kwani wabunge hawapo nyuma katika kufanya maendeleo.

Katika hatua nyingine, Katibu wa UWT Mkoa wa Shinyanga, Asha Kitandala akiwa na wajumbe wa baraza hilo waliokuwa wakikagua ujenzi wa nyumba ya katibu wa UWT inayojengwa Bushushu kata ya Lubaga amesema ujenzi huo umeanza leo na utachukua siku 16.

"Niwaombe kina mama kama alivyosema mwenyekiti wetu kweli tupendane niombe tushirikiane na wabunge wetu wote na tuwapende ili tuweze kufanya vitu vizuri tusibaguane na kuchongeana,

“Shinyanga tushikamane, wabunge wetu wamechangia fedha nyingi katika ujenzi huu, ambapo Lucy Mayenga kachangia Sh1 milioni na Santiel kachangia Sh1 milioni na wabunge wengine watatoa tuendelee kushirikiana nao,”amesema Kitandala

Mjumbe wa baraza la UWT Taifa, Christina Gule amewaomba wanawake kuendelea kuwa na ushirikiano ili waweze kufanya mambo makubwa ndani ya CCM na kutatua kero mbalimbali wakishirikiana na wabunge katika kuinua maendeleo ya jumuiya na chama hicho.

“Ni heshima kubwa kuanzisha ujenzi huu kwani toka ianzishwe UWT Mkoa wa Shinyanga haijawahi kujengwa  nyumba ya katibu na sasa tunaendelea kujenga tunashukuru chama mkoa kwa kuendelea kutusapoti na tunawashukuru wabunge wetu kwa kuendele kutushika mkono tumeanza leo kujenga, niwaombe wajumbe wa baraza tuendelee kutafuta fedha ili nyumba hii imalizike kwa wakati,"amesema Gule

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments