Sh bilioni 50 kuimarisha miundombinu ya mawasiliano

SERIKALI imesaini mkataba wa Sh bilioni 50 na muungano wa kampuni za huduma za mawasiliano kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya mawasiliano nchini.

Hafla ya utiaji saini imefanyika leo jijini Dar es Salaam kati ya Wizara ya Habari, Mawasiliano, na Teknolojia ya Habari na Muungano wa Watoa Huduma za Mawasiliano (Consortium of Telco Operators) ambao ni Airtel, Honora (Tigo) na Vodacom.

Aidha, watoa huduma hao wameahidi kuwekeza Sh bilioni 32.5 katika maendeleo ya miundombinu nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Waziri wa Habari, Mawasiliano, na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amesisitiza dhamira ya serikali katika kuhakikisha Tehama inakuwa kichocheo cha ukuaji wa kiuchumi nchini.

Katika tukio hilo ambalo lilihusisha utiaji saini wa nyaraka mbili muhimu hati ya maridhiano na hati ya mkataba wa nyongeza, Waziri Nape amesema serikali inaendelea kusimamia kwa ukaribu kuhakikisha huduma za Tehama zinawafikia Watanzania wote.

Makubaliano haya ya kihistoria yaliyoanza Oktoba 4,2011, kati ya serikali na kampuni hizo yalilenga kuimarisha miundombinu ya mawasiliano nchini, yamejikita katika ujenzi wa Mtandao wa Optiki (Optic Fibre Cable Network) katika maeneo yaliyokuwa hayajafikiwa na mtandao wa Mkongo wa Taifa.

Waziri Nnauye alisisitiza dhamira ya serikali ya kuimarisha upatikanaji na ubora wa huduma za mawasiliano nchini. Aliainisha hatua za hivi karibuni kama ujenzi wa minara ya mawasiliano 758 ili kupanua wigo wa huduma kwa zaidi ya Watanzania milioni nane na kupunguza gharama za ufungaji wa miundombinu ili kuharakisha utoaji wa huduma za mawasiliano unakuwa nafuu na bora zaidi.

Aidha, serikali imeongeza uwezo wa mtandao wa mawasiliano wa Mkongo wa Taifa kutoka 200Gbps hadi 800Gbps na ina mipango ya kuufikisha 2Tbps. Ujenzi wa mtandao wa Mkongo wa Taifa unaendelea kujengwa na unatarajiwa kufikia wilaya 99 kati ya 139 ifikapo Machi 2024, na lengo la kufikia wilaya zote ifikapo mwishoni mwaka 2024.

Waziri Nape alisisitiza kuwa kuimarisha sekta ya Tehama na kutachochea maendeleo ya kiuchumi, kukuza biashara, na kuongeza uchumi wa kidijitali kwa maendeleo ya kijamii. Lengo la serikali ni kuhakikisha kuwa 85% ya Watanzania wanapata intaneti ya kasi ifikapo 2025.

Hata hivyo, Nape alimshukuru na kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan, katika jitihada za kukuza Sekta ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) nchini.

Nape pia alimpongeza Adolf Ndunguru, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais TAMISEMI, na Mwenyekiti wa Timu ya Serikali ya Majadiliano kwa uongozi wake. Pia amempongeza, Mohammed Khamis Abdulla, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano, na Teknolojia ya Habari, kwa usimamizi wake bora katika kufikia makubaliano makubaliano hayo muhimu kwa sekta ya mawasiliano nchini.

Alitoa maelekezo kwa utekelezaji mzuri wa makubaliano hayo, akisisitiza umuhimu wa haraka katika kukamilisha mkataba wa uwekezaji. Pia aliwaomba Wizara, Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), na Muungano wa Watoa Huduma kuhitimisha mkataba wa haki ya matumizi na kuhakikisha kuwa miundombinu ya mawasiliano inatumika kwa ufanisi na usawa kama ilivyokusudiwa.

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments