DKT. NCHEMBA AISHAURI ANGLO GOLD ASHANTI KUIUZIA DHAHABU BENKI KUU YA TANZANIA

WAZIRI wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, ameushauri uongozi wa Kampuni ya Uchimbaji Dhahabu ya Anglo Gold Ashanti, inayomiliki Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine-GGM), kuanza kuiuzia Serikali dhahabu kupitia Benki Kuu ya Tanzania ili kuiwezesha Serikali kuhifadhi dhahabu kama akiba ya fedha za kigeni.

Dkt. Nchemba ametoa ushauri huo Jijini Dodoma alipokutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mkuu wa masuala ya Fedha wa Kampuni hiyo, Bi. Gillian Doran, ambapo wamejadili masuala kadhaa ya ushirikiano kati ya Kampuni hiyo na Serikali.

Alisema kuwa hatua hiyo itaifanya Serikali kuwa na chanzo cha uhakika cha kupata dhahabu pamoja na kuwatumia wachimbaji wadogo ambao hivi sasa ndio wanaofanyabiashara ya kuiuzia dhahabu Benki Kuu ya Tanzania.

“Lengo la hatua ya Serikali ya kuanza kuhifadhi dhahabu kama fedha za kigeni ni kuifanya nchi kuwa na chanzo cha uhakika cha fedha za kigeni kitakachotumika kama dhamana wakati inapohitaji fedha hizo kwa ajili ya matumizi mbalimbali badala ya kutegemea mikopo” alisema Dkt. Nchemba.

Aidha, Dkt. Nchemba alisema kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameilekeza Wizara ya Fedha kuanza kununua dhahabu na kuitunza kama fedha za kigeni, maelekezo ambayo tumeyatekeleza na Benki Kuu imeanza kununua dhahabu.

“Akiba ya Dhahabu itatusaidia kununua bidhaa muhimu zitakazokuwa zinahitajika nchini ikiwemo mafuta na bidhaa nyingine, wakati wa changamoto ya upatikanaji wa fedha za kigeni na hatua hii inafaida kubwa kiuchumi” alisisitiza Dkt. Nchemba

Vilevile Dkt. Nchemba alisema kuwa mitambo ya kuchenjua dhahabu iliyojengwa Geita na Mwanza, itakuwa na manufaa endapo dhahabu inayozalishwa nchini itachakatwa na kuongezwa thamani hapa hapa nchini na kuchangia pato la Taifa.


Katika Mwaka wa Fedha 2023/2024, Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imejipanga kununua tani sita za dhahabu kwa ajili ya kuweka akiba katika mfumo wa fedha za kigeni.

Kwa upande wake, Afisa Mkuu wa masuala ya Fedha wa Kampuni ya Anglo Gold Ashanti, Bi. Gillian Doran, aliipongeza Serikali kwa kuweka mazingira mazuri ya ufanyaji biashara na kuahidi kuwa itaimarisha zaidi ushirikiano na Serikali kupanua uzalishaji wa madini nchini.

Aliahidi kuufanyia kazi ushauri uliotolewa wa kuiuzia Serikali dhahabu kama njia ya kutunza fedha za kigeni lakini pia kuendelea kusaidia huduma za kijamii katika aneo la mgodi wa dhahabu wa Geita kwa manufaa ya wananchi.

WAZIRI wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb)(kulia), akisalimiana na Afisa Mkuu wa masuala ya Fedha wa Kampuni ya Uchimbaji Dhahabu ya Anglo Gold Ashanti, inayomiliki Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine-GGM), Bi. Gillian Doran, walipokutana kujadili masuala kadhaa ya ushirikiano kati ya Kampuni hiyo na Serikali, jijini Dodoma.


WAZIRI wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb)(katikati), akimshuhudia Afisa Mkuu wa masuala ya Fedha wa Kampuni ya Uchimbaji Dhahabu ya Anglo Gold Ashanti, inayomiliki Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine-GGM), Bi. Gillian Doran (Kushoto), akisaini kitabu cha wageni, wakati uongozi wa kampuni hiyo ulipomtembelea jijini Dodoma, ambapo wamejadili masuala kadhaa ya ushirikiano kati ya Kampuni hiyo na Serikali.


WAZIRI wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) ( wa tatu kulia), akiagana na Afisa Mkuu wa masuala ya Fedha wa Kampuni ya Uchimbaji Dhahabu ya Anglo Gold Ashanti, inayomiliki Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine-GGM), Bi. Gillian Doran (wanne kushoto), baada ya kumalizika kwa kikao kati ya Serikali na Kampuni hiyo ambapo wamezungumza masuala kadhaa ya ushirikiano kati ya Kampuni hiyo na Serikali, jijini Dodoma. Wengine katika picha ni Kamishna wa Sera Wizara ya Fedha, Bw. William Mhoja (wa pili kulia), Makamu wa Raisi wa Kampuni ya GGM, Bw. Simon Shayo (wa tatu kushoto) na Kamishna Msaidizi wa Sera Wizara ya Fedha, Bw. Cyril Chimilila (kulia).

WAZIRI wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) ( wa tatu kulia), na Afisa Mkuu wa masuala ya Fedha wa Kampuni ya Uchimbaji Dhahabu ya Anglo Gold Ashanti, inayomiliki Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine-GGM), Bi. Gillian Doran (wanne kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kumalizika kwa kikao kati ya Serikali na Kampuni hiyo ambapo wamezungumza masuala kadhaa ya ushirikiano kati ya Kampuni hiyo na Serikali, jijini Dodoma. Wengine katika picha ni Kamishna wa Sera Wizara ya Fedha, Bw. William Mhoja (wa pili kulia), Makamu wa Raisi wa Geita Gold Mine, Bw. Simon Shayo (wa tatu kushoto) na Kamishna Msaidizi wa Sera Wizara ya Fedha, Bw. Cyril Chimilila (kulia).

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma) 

#VIDEO: Wananchi Mkoani Singida Wametakiwa Kuendelea Kutoa Taarifa Kwa Jeshi La Polisi

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments