DODOMA: NAIBU Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Deogratius Ndejembi amesema vikundi 102 vya Wanawake vyenye wanufaika 875 vinavyojishughulisha na kazi za ufugaji vimekopeshwa kiasi cha Sh milioni 575.
Ndejembi ameyasema hayo leo Februari 2, 2024 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mwantum Zodo aliyehoji Serikali ina mpango gani wa kuvisaidia vikundi vya uzalishaji mali vikiwemo vya ufugaji ambavyo wanawake wamehamasika ili waweze kufanya ufugaji wenye tija.
Amesema Halmashauri za Mkoa wa Tanga na maeneo mengine nchini zimekua zikitoa mikopo ya uwezeshaji kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani.
Ndejembi amesema mikopo hiyo imekua ikitumika kwenye shughuli mbalimbali za uzalishaji ikiwemo ufugaji.
“ Kwa mwaka wa fedha 2021/22 na 2022/23, mikopo ya halmashauri ina thamani ya Sh bilioni 4.5 ambapo kati ya fedha hizo Sh bilioni 1.8 zilikopeshwa kwenye vikundi vya wanawake,” amesema Ndejembi.
0 Comments