WAZIRI JAFO ASHEREHEKEA SIKU YA KUZALIWA KWA KUPANDA MTI

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo amewahimiza Watanzania kuendelea kutunza na kuhifadhi mazingira ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.


Amesema suala la hifadhi ya mazingira ni ajenda muhimu hivyo kila mwananchi anao wajibu wa kupanda miti na kuitunza ili kulinda mazingira.

Dkt. Jafo ametoa kauli hiyo wakati alipojumuika na wanafunzi wa Shule ya Msingi Tabata JICA jijini Dar es Salaam katika zoezi la upandaji wa miti kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa

Akizungumza mara baada ya kuongoza zoezi hilo la upandaji wa miti, amewahimiza wananchi kuwa na utamaduni wa kupanda miti wanaposherehekea siku ya kuzaliwa ili kulinda mazingira.

“Nimefarijika sana kwa zoezi hili la upandaji wa miti kupitia Taasisi hii ya My Birthday Tree kutoka Morogoro na wenzetu wa Azam Media kwa kuunga mkono Serikali kupanda miti pamoja na wanafunzi na mkuu wa shule na walimu wa shule hii,” amesema.

Ameongeza kuwa kwa mujibu wa sensa ya wat una makazi ya mwaka 2022 Watanzania zaidi ya milioni 60 wakipanda miti nchi itakuwa na idadi kubwa ya miti ambayo ikistawi italeta tija.

Aidha, Waziri Dkt. Jafo amesema kuwa zoezi hilo la upandaji wa miti ni katika kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa ni kinara wa mazingira.

Halikadhalika Dkt. Jafo amesema Serikali imezindua kampeni mbalimbali za upandaji wa miti ili kuifanya Tanzania kuwa ya kijani na hivyo kukabiliana na changamoto za kimazingira.

Ametumia nafasi hiyo pia kuwaomba Watanzania kuunga mkono ajenda ya nishati safi ya kupikia na kuachana na kuni na mkaa ili kupunguza ukataji wa miti kwa hatua inayochangia uharibifu wa mazingira.

Kwa upande wa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya My Birthday Tree Bw. Festo Mwandenene ameishukuru na kuipongeza Serikali kupitia viongozi kwa hamasa yao ya kupanda miti.

Amesema hatua hiyo ni chachu kwa kuweza kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika kuhifadhi mazingira huku akitoa hamasa kwa wananchi kutumia siku ya kuzaliwa kupanda miti.

Itakumbukwa Waziri Dkt. Jafo mwaka 2023 alitoa wito kwa Watanzania kutumia siku yao kuzaliwa kuzaliwa kwa kupanda miti hatua iliyoleta chachu kwa wadau kuhamasika kupanda miti.





TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments