MADIWANI KALIUA WAPITISHA MAPENDEKEZO YA BAJETI YA BILIONI 40.7 KWA MWAKA 2021/22MADIWANI KALIUA WAPITISHA MAPENDEKEZO YA BAJETI YA BILIONI 40.7 KWA MWAKA 2021/22

 HALMASHAURI ya Wilaya ya Kaliua inakadiria kukusanya mapato na kutumia jumla ya shilingi bilioni 40.7 katika mwaka ujao wa fedha.

Kauli hiyo imetolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua Jerry Mwaga wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani cha kupitia mapendekezo mpango na bajeti ya 2021/22.

Alisema kati ya fedha hizo , wanatarajia kupata kiasi cha bilioni 36.6 kutoka Serikali kuu, kiasi cha bilioni 3.4 kutokana na mapato ya ndani na kutoka kwa wahisani wanatarajia kupata kiasi cha milioni 609.

Mwaga alisema kuwa bajeti ijayo imezingatia uboreshaji wa miundombinu ya elimu, afya , kuboresha huduma za ugani wa sekta ya mifugo na kilimo ili kuongeza uzalishaji na kuinua uchumi wa wakulima na wafugaji.

Alisema kuwa mambo mengine muhimu ambayo wamezingatia ni kuandaa mipango ya matumuzi bora ya ardhi na kutenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji kwenye masuala ya viwanda, biashara, michezo na maeneo kwa ajili ya wakulima na wafugaji.

Mwaga aliongeza kuwa eneo jingine ni kuendelea kuwahamasisha wananchi kuanzisha na kujiunga na kuimarisha vyama vya ushirika (AMCOS, SACCOS na VICOBA).
Alisema pia wamepanga kuongeza juhudi katika ukusanyaji mapato ya ndani kwa kutumia mfumo wa kielektroniki na kuimarisha miundombinu ya kudhibiti taka ngumu na majitaka.

Akifunga kikao hicho baada ya Madiwani kupitisha, Mwenyekiti wa Halmshauri ya Wilaya ya Kaliua Japhael Lufungija alisema mapendekezo yao yakipitishwa yawatasaidia kupeleka huduma mbalimbali ikiwemo za afya, elimu , ugani na shughuli mbalimbali za maendeleo kwa wananchi.

Alisema mapendekezo ya bajeti ijayo yamekita pia katika kuongeza nguvu kwa kubuni vyanzo vipya vya mapato ambavyo vitawasaidia kupata fedha kwa ajili ya kuboresha huduma za wananchi wa Kaliua.

Aidha Lufungija alisema kati ya mapendekezo yao kiasi cha shilingi bilioni 9.3 kwa ajili ya miradi mbalimbali ya ya maendeleo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Kaliua Jerry Mwaga(kushoto) akijibu maswali ya Madiwani jana wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani cha kupitia mapendekezo mpango na bajeti ya 2021/22. Wengine katika picha ni Mwenyekiti w Halmashauri hiyo Japhael Lufungija(katikati) na Mbunge w Jimbo la Ulyankulu Rehema Migila(kulia)
Baadhi ya Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua na Wakuu wa Idara na Vitengo wakiwa jana katika kikao cha Baraza la Madiwani cha kupitia mapendekezo mpango na bajeti ya 2021/22.
Mwenyekiti wa Halmshauri ya Wilaya ya Kaliua Japhael Lufungija(Katikati) akifunga jana kikao cha Baraza la Madiwani ambacho kilipitisha mapendekezo mpango na bajeti ya 2021/22 ya shilingi bilioni 40.
Na Tiganya Vincent, Tabora

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments