Kisa cha Mrema kutimuliwa uwaziri, kuwania urais kupitia NCCR

Katika toleo lililopita tuliona jinsi Augustine Mrema alivyopaa kisiasa mara baada ya kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani.

Kupaa huko kuliongezeka alipozima mgogoro wa Kanisa la KKKT Dayosisi ya Arumeru na Rais Ali Hassan Mwinyi akampa cheo cha naibu waziri mkuu ambacho hakikuwapo kikatiba.

Umaarufu wa Mrema ulipanda kutokana na aina yake ya utendaji ambayo ilimfanya hata akaingilia utendaji kazi wa wengine, akiamini kwamba watendaji hao walikuwa hawafanyi kazi inavyotakiwa na kuwa mambo ya ndani ni kila kitu.

Pamoja na hayo, Mrema aliitumikia wizara hiyo kwa miaka minne hadi alipoondolewa wakati wa mabadiliko ya Baraza la Mawaziri yaliyofanywa na Rais Mwinyi Jumatano ya Desemba 7, 1994.

Katika mabadiliko hayo, Mrema alipelekwa katika Wizara ya Kazi, Maendeleo ya Vijana na Michezo.

Katika wizara hiyo mpya alidumu kwa siku 79 kuanzia Desemba 7, 1994 hadi Februari 24, 1995, saa chache kabla Rais Ali Hassan Mwinyi hajatangaza kumfukuza uwaziri.

Tukio lililoibua mzozo kati ya Mrema na Rais Mwinyi ni mjadala bungeni Dodoma baada ya kuwasilishwa Ripoti ya Kamati ya Bunge kuhusu masuala ya mfanyabiashara maarufu raia wa kigeni aliyekuwa mmiliki wa mashamba kadhaa ya mkonge, Vidyadhar Girdharlal (V.G.) Chavda, jambo ambalo lilikuwa limetamba kwenye vyombo vya habari kwa miezi mingi.

Kamati ilipendekeza kukamatwa na kufunguliwa mashtaka kwa V.G. Chavda kutokana na kashfa ya mamilioni ya fedha za kigeni.

Kamati ilidai kuwa Chavda alitumia vibaya Sh916 milioni katika fedha za kubadilisha deni alilokopeshwa na Serikali kuendeleza mashamba manne ya mkonge aliyokuwa akimiliki.

Baadhi ya mawaziri walieleza kwamba Chavda hakuwa na hatia, lakini Februari 11 Serikali ilimtangaza kuwa mhamiaji aliyepigwa marufuku. Siku tatu baadaye Mahakama Kuu iliizuia Serikali kumfukuza nchini.

Mrema alitumia nafasi hiyo kuishutumu Serikali ambayo yeye alikuwa sehemu yake.

Alisema bungeni kuwa dhamiri yake ingemsumbua endapo angekubaliana na Serikali kwenye suala la Chavda.

Kutokana na msimamo huo, Rais Mwinyi alimfuta kazi kwa kushindwa kuzingatia uwajibikaji wa pamoja.

Hata leo, katika kumbukumbu ya matukio hayo, Mrema anasema kutokana na uadilifu aliokuwa nao isingekuwa rahisi kwake kunyamazia suala la ubadhirifu wa fedha za mkonge kwa wajanja wachache, akiwamo V.G. Chavda.

Akikumbuka hayo, Mrema anasema “nchi ilikuwa inaibiwa, nilisikia uchungu sana. Nilikuwa napambana mwenyewe. Haukuwa msukumo wa Serikali, ni Mrema pekee.”

Mrema anasema hata hivyo hilo halikumnyima usingizi, badala yake aliamua kupambana na kuhakikisha mfanyabiashara huyo anafikishwa katika vyombo vya dola.


Atimkia upinzani

Katika mahojiano maalumu na gazeti hili aliyofanyiwa Machi 2018, Mrema anasema licha ya kufanya kazi vizuri akiwa CCM, siku moja aliona ni busara kukihama chama hicho na kutimkia upinzani ili aweze kutimiza kile alichokiamini.

“Siwezi kusema nilinyanyasika CCM. Rais Mwinyi alikuwa ananipenda sana kutokana na utendaji wangu, lakini ukweli ni kwamba watu wanaishi kwa malengo. Pale nilipokuwa nimefika nisingefanya zaidi. Nikajiuliza mbona nina uwezo zaidi kwa nini nang’ang’ania huku? ... Nina marafiki, wakasema kama CCM hawawezi kukupa nafasi ya kufanya zaidi kwa nini usiondoke, nikaamua kufanya maamuzi,” alieleza Mrema.

Muda mfupi baadaye, Mrema alitangaza kuwa kwa vile ‘ananyanyaswa’ na chama tawala (CCM), Ijumaa Machi 4, 1995, alitangaza kujitoa CCM.

Kutokana na uamuzi huo, alikoma kuwa mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano.

Alisema hakuwa na nia ya kuondoka CCM, lakini Serikali ilifika wakati haitawali tena na ilikuwepo ‘clique’ (kakundi) ndani ya Serikali inayoshirikiana na Chavda.

“Nilitarajia CCM ingejitokeza kunipongeza kwa hatua hiyo kwa sababu mimi ni kada wake na ilinituma serikalini kusimamia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi na nikiwa pia katibu mwenezi wa CCM Moshi Vijijini. Nasikitika CCM haikufanya hivyo ... Aliniita (Laurence) Gama (katibu mkuu wa CCM wakati huo) kutaka kujua ikiwa bado niko CCM au natoka ... CCM si mama wala baba yangu. Ni sera za kutetea wanyonge,” alisema Mrema.

Siku kumi baadaye, Jumanne ya Machi 14, 1995, Rais wa kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere, alitoa hotuba ambayo pamoja na mambo mengine, alisema “Tanzania inanuka rushwa.”

Siku moja baadaye Mrema alijiunga na NCCR-Mageuzi Jumatano Machi 15, 1995.

Kwa Mrema kujiondoa CCM na kujiunga na NCCR-Mageuzi lilikuwa tukio la kihistoria lililobadili siasa za upinzani hapa nchini.

Alipoanza mikutano ya kisiasa akiwa katika chama chake kipya, mikutano yake mingi ilipigwa mabomu ya machozi na polisi.

Tangu kuruhusiwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, Tanzania ilikuwa haijawahi kuona mwanasiasa wa upinzani mwenye nguvu na ushawishi kama Mrema anahama CCM na kuleta mtikisiko.

Mrema alipohama CCM, karibu vyama vyote vilivyopata usajili nchini vilimwomba ajiunge navyo. Kila chama kilikuwa na uhakika wa kuongeza idadi ya wanachama iwapo vingempata mwanasiasa huyo.

Mmoja wa watu waliohusika na jitihada za kumhamishia Mrema kutoka CCM kwenda NCCR-Mageuzi alikuwa ni Msafiri Mtemelwa, ambaye wakati huo alikuwa mwenyekiti wa umoja wa vijana wa chama hicho.

“Mrema alikuwa anatisha wakati huo. Kabla hajajiunga na chama chetu, tulikuwa chama kizuri, lakini hatukuwa na wafuasi kabisa. Nakumbuka kuna mikutano ya hadhara tulikuwa tunafanya na unakuta hujapata hata watu kumi.

Hadi wakati wa Uchaguzi Mkuu wa kwanza wa vyama vingi uliofanyika Jumapili ya Oktoba 29, 1995, idadi ya Watanzania ilikuwa ni 30,337,000. Kulingana na jarida ‘Elections Today’ la Januari 1996 (uk. 46), waliojiandikisha kupiga kura katika uchaguzi huo walikuwa 8,929,969. Idadi hiyo ilivunja rekodi za chaguzi nyingine zote zilizotangulia.

Katika uchaguzi mkuu wa mwisho chini ya chama kimoja cha siasa uliofanyika Jumapili ya Oktoba 28, 1990, idadi ya Watanzania ilikuwa ni 25,635,000 na waliojiandikisha kupiga kura walikuwa ni 7,296,553, lakini waliojitokeza ni asilimia 74 tu, yaani wapiga kura 5,425,282. Kura za NDIYO zilikuwa 5,198,120 na za HAPANA ni 117,366.

Kwa mwaka aliogombea Mrema wa 1995, ingawa waliojiandikisha kupiga kura walikuwa 8,929,969, waliojitokeza kupiga kura ni 6,846,681, ambao ni sawa na asilimia 76.7 ya waliojiandikisha. Ingawa uchaguzi katika majimbo saba ya Mkoa wa Dar es Salaam ulisimamishwa na kisha ukafanyika Novemba 19 ya mwaka huo, haukuathiri ushindi wa CCM.

Wagombea urais katika uchaguzi huo walikuwa ni Benjamin Mkapa (CCM) aliyepata kura 4,026,422 (61.82%), Augustine Mrema (NCCR-Mageuzi) kura 1,808,616 (27.77%), Profesa Ibrahim Lipumba (CUF) kura 418,973 (6.43%) na John Cheyo (UDP) kura 258,734 (3.97%).

Je, nini kilitokea hadi akagombea ubunge Jimbo la Temeke? Tukutane toleo lijalo.

 

TUANDIKIE MAONI YAKO HAPA CHINI

Je, wewe ni Mfanyabiashara na Unatamani Kutangaza Bidhaa Zako Kupitia Tovuti/Blog Yetu? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia bandolaonline@gmail.com au WhatsaApp: + 255 766 365 560 au 0652 388 516

Post a Comment

0 Comments