Hapi Ataka Vijana Waandaliwe Kuongoza

Mkuu wa mkoa wa Mara, Ally Hapi ameiomba serikali kuwa na mpango wa kuwaandaa vijana  kushika nafasi mbalimbali za uongozi za ndani ya Serikali na chama.

Pia ametoa wito wa kutolewa mafunzo ya uzalendo, maadili na uongozi ili kuwafanya vijana wawe na mchango katika ujenzi wa taifa.

Hapi ametoa wito huo leo katika kumbukumbu ya miaka 100 ya kuzaliwa kwa hayati Julius Nyerere (Baba wa Taifa) huku akisema iwapo vijana hao wakijengewa uwezo na kupewa maarifa watakuwa na mchango kama ambavyo Nyerere aliongoza jitihada za kuleta uhuru akiwa na umri wa miaka 39.

"Baba wa taifa alikuwa kijana lakini aliweza kusimama na kutoa uongozi kwa taifa, wazee na viongozi waliokuwepo wakamsikiliza na kumuelewa hii ni kwa sababu aliandaliwa," amesema Hapi

Ameongeza kwamba pamoja na viongozi wa sasa kufanya kazi nzuri lakini pia Chuo cha Utumishi wa Umma kilichopo Kibaha mkoani Pwani kina kazi ya ziada ya kuwaandaa vijana kurithi mikoba ya uongozi nchini.

 

Post a Comment

0 Comments